Saturday, February 4, 2017

WITO WA KUZIMU SEHEMU YA TATU










WITO WA KUZIMU

NA: HASSAN O MAMBOSASA

MAHALI:TANZANIA


SIMU:+255713776843
      +255762219759

WHATSAPP:+255713776843
         +255762 219759

BLOG: riwayamaridhawa.blogspot.com





SEHEMU YA TATU!!
Mlango wa sehemu ya maakuli  ulimvutia sana kuutazama na akajikuta kabisa akivutika kuusogelea pia ingawa kimuonekano ulikuwa hauvutii kabisa kwa jinsi ulivyoungua, alijikuta akipiga hatua kuelekea eneo hilo la jikoni ambapo kulikuwa kumemvutia sana.






________________TIRIRIKA NAYO
   Mwanga wa kurunzi ukiwa upo mbele yeye nyuma hadi ndani ya chumba hicho cha jiko ambacho hakikuwa kisichotamanika hata kukitazama kwa mtu aliyekuwa akiyajua mandhari ya hapo jikoni kabla ya kutokea kwa tukio , Mutonga alibaki akiyatazama mandhari ya jiko hilo ambalo lilionekana lilikuwa ni la kisasa sana kabla hata halijakumbwa na tukio  la kulipuka. Muale wa Kurunzi ulimsaidia kuona mambo mbalimbali yaliyokuwa humo jikoni ambayo mengine kwa asilimia kubwa yalikuwa na masizi ya kuungua, sehemu ya jiko ambazo hazikuwa zimejengwa kwa malighafi yenye kuungua na moto bado zilikuwa zimebaki  majivu matupu huku zile zilizokuwa zimejengwa na miti migumu zikiwa hazina tofauti na mkaa. Mutonga akiwa humo jikoni aliweza kushuhudia mitungi mitatu ya gesi ikiwa imetoboa ukuta sehemu za mbele na nyuma sehemu za nyuma za mitungi hiyo zikiwa zimebaki humo ndani ya jiko.


  Alipoona mitungi hiyo ndipo alipoweza kutambua kuwa mlipuko uliotokea ndani ya nyumba hiyo haukuwa mkubwa sana, mitungi hiyo ilimbainishia kuwa hiyo ndiyo iliyoongeza mlipuko  humo ndani na kuufanya uwe mkubwa sana. Alinyanyua kichwa na kukishusha kuafiki mawazo yake hayo na kisha akatembeza Kurunzi kuangalia katika pande nyingine za ndani ya chumba hiko cha jiko. Hakuweza kushuhudia kabisa kitu kingine ndani ya jiko hilo, ilimbidi atoke humo jikoni baada ya kuona hakukuwa na cha maana. Alipomulika kurunzi yake sehemu ya mlangoni wakati wa kutoka alijikuta akisita baada ya miale ya kurunzi yake kutua mahali tofauti na alivyoingia. Miale ya Kurunzi kipindi anaingia akiwa yupo sebuleni aliweza kuliona jiko kwa ndani bila ya kuwepo kwa kizuizi chochote lakini muda huu hapo kwenye kizingiti cha jiko aliona kizuizi kilichokuwa kikizuia miale ya Kurunzi hiyo isiweze kufika sebuleni. Kizuizi hicho hakikuwepo kabisa na wala hakikuwa kimeinyima miale ya Kurunzi yake uhuru wa kufika mbele zaidi.

  Kizuizi alichokiona mbele yake kilikuwa ni kizuiaji kilicho na uhai na chenye sifa sawa na yeye, Kizuizi hiko kilikuwa ni sifa za mafichoni tofauti na yeye tu ndiyo kilimfanya awe tofauti na yeye kwa hilo tu. Kizuizi hiko chenye mvuto kikiwa kimeacha asilimia kubwa ya vitu vyake vyenye mvuto wazi ndiyo kilionekana hapo mbele yake kikiwa kimezuia miale hiyo ya Kurunzi yake isiweze kufika mbele zaidi alipojaribu kumulika. Hakika alikuwa ni binadamu kama yeye tena mwenye jinsia ya kike tofauti na yeye, alikuwa amesimama mbele tu akimtazama yeye kama aliyekuwa akitarajia ujio wake mahala hapo. Mwanamke huyo alikuwa amevaa kaptula fupi sana ambayo iliacha sehemu ya mapaja yake yaliyojaa nje ndiyo alionekana hapo akiwa amesimama tena akimtazama yeye jinsi alivyokuwa akimuangalia. Alionekana wazi huyo mwanamke alikuwa akimtazama kwa muda mrefu sana tangu alipokuwa akimulika humo ndani kupekua lakini hakumuona hadi hapo alipokuwa akitaka kutoka humo ndani, Mutonga alishtuka san kutokana na ughafla wa ujio wa mwanamke huyo. Ilimchukua sekunde kadhaa kumzoea baada ya kumuona ni mwanadamua wa kawaida, pamoja na kumzoea huko bado alikuwa na maswali kichwani mwake juuu ya ujio wake mahala hapo ambao haukuwa wa kawaida kabisa. Hakukuwa na kiumbe yeyote aliyekuwa ameruhusiwa kuingia humo ndani na  Askari aliyekuwa langoni lakini huyu mwanamke alifika hadi ndani haikueleweka aliingia vipi, kiupande mwingine aliona ni kama uzembe wa askari aliyekuwa akilinda hapo mlangoni. Ilimbidi apate uhakika tu wa huyo mwanamke kuwemo humo ndani, ndipo aweze kujua kuwa alikuwa humo ndani kwa muda gani na nani kamruhusu aingie.

"Unafuata nini huku?" Mutonga aliuliza

"Wewe hapo ndiyo nimekufuata na si kingine" Mwanamke huyo alijibu

"Hey usilete mchezo we binti hebu toka nje haraka iwezekanavyo"

"Sitoki mpaka nipate nilichokifuata"

"Ok unachokitaka ni nini we binti katulie na mumeo au bwana wako si huku kwenye kazi za watu"

"Roho yako tu si kingine maana inaonekana unafuatilia kile usichokijua mwanzo wala kati yake"

"Nini wewe?"

  Swali lake hilo halikujibiwa hata kidogo kwani yule Mwanamke alifyatuka pale alipokuwa amekaa, alikuja na mapigo ya karate ya namna tofauti ambayo yalimuwia vigumu sana Mutonga kuyazuia yote. Mengi ya mapigo hayo yalimuishia mwilini mwake na kumfanya aende chini moja kwa moja. Kurunzi ambayo ilimuwezesha kumuona Mwanamke haikuwepo tena kwenye mkono wake tayari ilisharuka mbali sana na ikawa inamulika ukutani na si katika eneo hilo alilokuwepo ambapo ingemuwezesha kumuona huyo Mwanamke aliyempiga mapigo ya ajabu mengi.  Giza nene lilikuwa katika eneo hilo alilokuwepo huyo mwanamke ambalo lilimzuia kabisa kuweza kumuona, akiwa yupo ndani ya Giza hilo Mutonga alishindwa kabisa kumuona Adui yake alikuwa yupo upande gani. Alijikuta tu akipokea kipigo cha haja ambacho kilimletea maumivu katika mwili wake ambayo yalimfanya hata atamani kupiga kelele. Alipofungua mdomo wake pale alipozidiwa na maumivu alijikuta akizuiwa, mikono ya Mwanamke huyo ilitua kwenye kinywa chake kumzuia huku akiendelea kumshushia kipigo. Kipigo kilidumu kwa muda mrefu ambacho kilimnyima kabisa Mutonga muda wa kujiteteta kwani uwepo wa giza ulikuwa umemnyima wasaa huo. Mwanamke huyo aliyekuwa akimpiga alionekana kabisa alikuwa akilimudu vyema giza hilo, hiyo ndiyo ilikuwa hatua kubwa aliyomzidi Mutonga katika mpambano huo. Ndani ya  muda mchache tu baadaye Mutonga hakuwa na nguvu hata ya kuweza kusimama kutokana na kuelemewa na kichapo  alichokuwa amepewa na huyo mwanamke, alikuwa hata hawezi  kujihami kutokana na kipigo hicho. Hapo alibaki akiwa anahema tu kama mkimbiaji wa mbio ndefu asie na pumzi, alibaki akikodoa macho ndani ya giza hilo asimuone Adui yake aliyempa kipigo cha namna hiyo hadi akawa hajiwezi.

"Malkia wa kuzimu haingiliwi kwenye kazi yake hata siku moja, haya na wewe ungana na Bai pamoja na Mabina katika kuelekea kuzimu bila ya kupata wito kama wao" Mwanamke huyo aliongea na kisha mlio wa kuvunjwa kwa kitu chenye mvupa mlaini kilisikika.


****



   Baada ya kushuka ndani ya ndege la shirika la ndege la Fastjet, Jeph hakutaka kupoteza aliamua kutoka ndani ya uwanja wa ndege wa hapo jijini Dodoma akiwa yupo na mkoba wake mdogo tu wa mabegani. Alikuwa ni mwenye kuvaa mavazi ya kileo kama ilivyo kawaida yake na alitembea kimaringo, macho yake yalikuwa yamefunikwa na miwani ya giza na alikuwa akitembea huku akiwa ameinamisha kichwa chake chini na kuufanya mkato wa nywele zake uliowekwa kiujana zaidi kuonekana kwa mtu yeyote aliyekuwa akipita mbele yake. Miondoko yake ya kiujana zaidi ambayo huweka manjonjo mengi zaidi  na kumfanya azidi kuvutia kila akitembea wala hakuiacha kabisa, ilikuwa ishajenga mazoea na sasa imekuwa ni tabia yake.

   Alitoka hadi nje kabisa ya uwanja huo baada ya kupitia kila eneo ambalo lilikuwa na utaratibu maalum uliotakiwa kupitiwa, alipotoka hadi nje hakutaka kupoteza muda kabisa aliagiza Teksi na akaondoka ndani ya eneo la uwanja wa ndege. Teksi hiyo ilimpeleka moja kwa moja hadi katikati ya jiji la Dodoma ambako alifikia kwenye hoteli maarufu sana jijini hapo, alichukua chumba kwenye hoteli hiyo na moja kwa moja akaenda chumbani kwake akiongozwa na Mhudumu wa hoteli hiyo.

  Alipoingia ndani ya hoteli hiyo haukupita hata muda mfupi mlango uligongwa, Jeph akiwa amevaa taulo tu alienda kuufungua mlango huo  ambako alikutana na yule Mhudumu aliyemleta humo ndani kwa mara ya kwanza. Mhudumu huyo alikuwa na Bahasha nyeupe mkononi mwake ambayo alimpatia, Jeph  aliipokea ile bahasha kisha akamtazama Mhudumu huyo wa hotelini usoni mwake kwa macho makali.

"Umeopata wapi hii?" Alimuuliza

"Kuna mkaka mmoja ameileta na ameteja hadi jina lako na chumba ulichokuwepo" Mhudumu alijibu na kupelekea Jeph agune kwani hakuwa amempa mtu yeyote taarifa za ujio wake ndani ya hoteli hiyo  zaidi tu ya watu wa  ngazi za juu waliokuwa wamempa kazi hiyo.

"Ok nashukuru" Ilimbidi amshukuru tu Mhudumu huyo kuweza kumuondoa ndani ya eneo hilo ndiyo aweze kuiangalia Bahasha  hiyo ilikuwa na kitu gani ndani yake, Mhudumu huyo alipoondoka ndani ya eneo hilo aliitazama Bahasha  kwa sekunde kadhaa kisha akaingia chumbani kwake na kufunga mlango.

   Alienda kujitupa kitandani na kisha mikono yake ikashika sehemu ya kufungulia Bahasha aliyoletewa, aliivuta sehemu ya kufungulia bahasha hiyo ndani akakutana na bahasha nyingine iliyokuwa haitofautiani kabisa na bahasha ambazo walizipokea Mheshimiwa  Bai na Mabina muda mfupi kabla ya vifo vyao. 'WITO WA KUZIMU' ndiyo neno lililokuwa lipo juu ya Bahasha ambalo lilimfanya afinye uso wake kama alikuwa akitazama kitu chenye umbo dogo kupitiliza. Taratibu alianza kushika sehemu ya Bahasha hiyo iliyokuwa imegandishwa kwa gundi imara na akaanza kuivuta, alijikuta  akisita kuifungua baada ya kusikia mlio wa Simu yake ya mkononi iliyokuwa ipo sentimita kadhaa kutoka hapo alipo. Jeph aliiweka bahasha hiyo kando na  akaichukua simu yake ya mkononi, aliitazama na akaona namba iliyokuwa ikimpigia iikuwa ni muhimu na aliipokea kwa haraka sana.

"Ndiyo Mheshimiwa....nimefika salama sasa hivi nipo hotelini napanga mipango....nashukuru Mheshimiwa sitakuangusha" Simu iliyokuwa imempigia ilikatika yeye akairudisha simu mahala pake ilipokuwa imejipumzisha baada ya yeye kuiweka na kisha akaishika Bahasha  kwa mara nyinyine kabisa, kwa haraka kabisa aliifungua bahasha hiyo kwani alikuwa na shauku ya kujua kile ambacho kilikuwa kipo ndani yake.


****


  
   Kishindo kizito kilisikika kwa ghafla nje ya hoteli maarufu sana jijini Dodoma, kishindo hiko kilitokea ghorofa ya pili ya hoteli hiyo kwenye chumba kimojawapo ambacho kilikuwa kimepata Mpangaji ndani ya muda mfupi  tena ikiwa haijafika hata nusu saa tangu  alipokilipia na kingia ndani ya chumba hicho. Mayowe ya watu waliokuwa wapo nje ya hoteli hiyo pamoja na ndani ya hoteli hiyo yalisikika kutokana na kushuhudia jinsi tukio hilo lilivyotokea. Walishuhudia mwanga mzito sana wa moto ukitokea kwenye dirisha la chumba cha hoteli ambao ulifanya hadi vioo vya dirisha kupasuliwa kwa nguvu sana na kuruka nje, watu waliokaa chini ya ghorofa la hoteli hiyo walikimbia wote baada ya fito la dirisha la hoteli hiyo kuwaangukia hapo chini walipokuwa wamekaa. Haikuchukua hata muda mrefu milango ya dharura ambayo hutumiwa kukiwa na moto ilisheheni watu waliokuwa ndani ya hoteli  ambao wote kwa pamoja walikuwa wakihangaika kuweza kuokoa maisha yao kutokana na dhahama  iliyotokea ndani ya hoteli hiyo ya kifahari. Wafanyakazi wa hoteli hiyo nao hawakuwa na ujasiri wa kuweza kuweza kubaki ndani ya hoteli yao, wote walijichanganya na wateja wa kawaida katika kukimbia balaa hilo katika jioni hiyo ambayo giza lilikuwa limeshaufukuza mwanga na kuchukua riziki yake.


   Ilichukua dakika takribani tano ndiyo vikosi vya uokoaji vya jeshi la polisi viliweza kuwasili ndani ya jengo hili na kuanza kazi yake, muda huo kwa msaada wa wahudumu waliokuwa wapo mapokezi waliweza kumtaja aliyekuwa yupo ndani ya cumba hicho ambaye ndiyo alikuwa na muda mchache tu tangu achukue chumba hicho hadi anakumbwa na mlipuko wa bomu . Polisi kwa muda huo wengine walikuwa wakishirikiana na wenzao wa zimamoto katika kuhakikisha kuwa moto huo unazimika upesi iwezekanavyo, magari ya kuzima moto yalianza kazi kwa mara moja katika kuhakikisha kuwa moto huo unazimwa haraka iwezekanavyo waweze kuokoa yule aliokuwa yupo ndani ya  chumba hicho.



****


   Muda huo kwa upande mwingine kabisa ndani ya eneo la Mwandege kata ya Vikindu nje  ya jiji la Dar es salaam katika Wilaya ya Mkuranga Mkoani Pwani, kijana asiyetambulika alileta barua katika nyumba moja ambayo ilikuwa ni ya kisasa ikiwa imejengwa mitaa kadhaa nyuma ya eneo la Mwandege Magengeni. Kijana huyo alijieleza kwa ufasaha kuwa alikuwa ametumwa kuleta barua  ndani ya nyumba aliyoifikia, alimkuta mwanamke wa makamo akiwa ndiyo huyo aliyemfungulia mlnago wa nyumba aliyoifikia. Mwanamke huyo alipopokea maelezo ya kijana huyo aliikubali barua hiyo na kisha akamshukuru kwa kufikisha hapo. Kijana  baada ya kuufikisha mzigo ambao alidai alikuwa ameagizwa hakutaka kupoteza muda aliondoka ndani eneo la hapo akarudi alipokuwa ametokea, alimuacha Mwanamke huyo ambaye aliambiwa mzigo huo ulikuwa ni wa mumewe akiutazma kwa shauku kubwa sana. Akiwa bado yupo kwenye lango kuu la magari la ndani ya nyumba yake aliishika Bahasha  nyeupe aliyoipokea ambayo haikuwa na alama yeyote ya uchafu akaifungua, wahka wa kutaka kujua kle kilichokuwa kipo ndani ya Bahasha  ndiyo ulimjaa huku akisahau kabisa kuwa Bahasha aliyoipokea haikuwa ikimuhusu kabisa zaidi ya yeye kuwa mfikishaji ujumbe kama yule Kijana aliyemletea. Mwanamke huyo kwakuwa muda huo mume wake aliyepaswa kuipokea Bahasha hakuwepo alijikuta akiifungua Bahasha isiyomuhusu akakutana na Bahasha nyingine ndani, kiherehere kilimzidi akajikuta akiisoma Mbebeo wa barua  aliokutana no kwa ndani ambao ulimfanya azidi kuwa kiherehere akajikuta akituliza macho yake kwenye Bahasha nyingine kabisa. Aliyasoma maandishi aliyokuwa yapo juu yake akiwa na macho yenye umakini mkubwa sana akajikuta akitokwa na mguno,pamoja na mguno huo alioutoa baada ya kusoma maandishi ya juu ya Bahasha hiyo ya pili iliyokuwa ipo ndani ambayo ilikuwa na mstari ya rangi nyekundu kama Bahasha zilizowahi kuwafikia Mheshimiwa Bai na Mabina. Bado hakusita kabisa kuifungua kabisa bahasha hiyo yeye ndiyo alipatwa na hamasa ya kutaka kuifungua wala hakujali kabisa uzito wa maneno hayo yaliyokuwa yapo juu ya bahasha yenyewe pamoja na mhuri wake wa kutisha. Hakuwahi kuiona pia stempu kama hiyo iliyokuwa imebandikwa juu ya bahasha hiyo lakini hilo hakujali kabisa yeye akili yake yote ilikuwa ipo kwenye kuifungua bahasha hiyo tu na si vinginevyo.


 Alishika bahasha hiyo kwa wahaka mkubwa sana wa kuifungua kabla ya mume wake hajarudi kwani hakuwa ameenda mbali kabisa, uwepo wa mume wake ulimfanya aharakishe katika kuifungua  kwa kuhofia huenda anaweza kumkuta na kwkuwaa hajajua kilichomo humo ndani yake wala kukisia. Papara ya kujua kile kilichokuwa kimo ndani ya mzigo uliomfikia ilikuwa ikimsumbua sana na wala hakuhofia kabisa kuwa papara hiyo ingeweza kumfanya hata apatwe na kile ambacho hakuwahi kupatwa nacho katika maisha yake yote. Yeye alichojali ni kuifungua tu  hiyo na kuangali ndani, wahka huo wa kuangalia kile ambacho kilikuwa hakimuhusu ulimfanya hata asahau tahadhari aliyowahi kupewa na Mume wake juu ya vitu kama hivyo vikija ndani ya nyumba hiyo ikiwa yeye hayupo ndani ya nyumba hiyo. Mwanamke huyo alishawahi kuonywa kabisa kuwa asifungue kitu  kitakacholetewa yeye ikiwa hamjui mletaji, onyo hilo alilipuuzia kabisa na wahka wa kutaka kujua kilichomo humo ndani ndiyo ukawa umelitangulia hatua kadhaa mbele onyo alilowahi kupewa na Mume wake. Alijikuta akiifungua kwa haraka na hata kabla hajaona kilichomo ndani yake mwanga mkali ulitoka  ulitoka ndani yake,hata kabla sekunde haijafika alijikuta akirushwa kwa nguvu huku akiteketea kwa moto na kwenda kujibamiza sehemu ya juu ya lango hilo na kisha baadhi ya viungo vyake vikatawanyika na kuruka upande tofauti. Huo ndiyo ulikuwa ni mwisho wa Mwanamama huyo aliyekuwa na wahka wa kufungua kile kilichokuwa hakimuhusu, mdharau mwiba  mguu huota tende na ndiyo hayo yaliyomkuta hapo mlangoni mwa nyumba yake umbali wa mita kadhaa kutoka mahali nyumba yake ilipo.

*UMBEA MBAYA
*CID WA PILI ANAANGMIA






ITAENDELEA!

No comments:

Post a Comment