Sunday, June 26, 2016

SHUJAA SEHEMU YA ISHIRINI NA TISA

RIWAYA: SHUJAA


MTUNZI: Hassan O Mambosasa

SIMU:+255713776843
+255762219759

WHATSAPP:+255713776843


SHUKRANI ZOTE ANASTAHIKI MWENYEZIMUNGU
MUUMBA WA DUNIA NA VILIVYOMO KWA KUNIPATIA
AFYA NJEMA ILIYONIWEZESHA KUANDIKA RIWAYA
HII KWA MARA NYINGINE




SEHEMU YA ISHIRINI NA TISA!!
"Poa" Moses aliitikia huku akizipokea funguo za gari, Hilary aliondoka akimuacha Moses akimaliza kujiandaa.

Moses alivaa nguo nyeusi ambazo zilimkaa vyema na alivaa kofia kubwa iliyomfunika sehemu kubwa ya uso wake kisha akafungua kabati la nguo akatawanya nguo, mlango mwingine ulionekana ambao pia aliufungua akaingia kisha akafunga mlango wa kabati kama ulivyokuwa awali na kurudishia nguo kama zilivyo. Aliufunga mlango wa pili pia baada ya kuingia ndani kabisa. Alishuka kwenye ngazi zilizopo humo ndani ya kabati hadi  chini kabisa ambapo taa zilikuwa zinawaka zilimsaidia kuongoza njia aliyokuwa anaelekea.




_________TIRIRIKA NAYO
Njia aliyoitumia Moses ilikuja kumfanya atokee katika upande mwingine kabisa wa mtaa wa Warioba ya uzio wa nyumba yao, baada ya kutoka nje tu alienda hadi pale alipokuwa ameelekezwa na Hilary kwenye nguzo ambapo alikuta gari hiyo aliyokuwa ameambiwa na rafiki yake kuwa ataikuta. Aliingia ndani ya gari hiyo na safari ikaanza mara moja kuelekea huko alipokuwa ametaka kwenda ndani ya muda huo, alizunguka mitaa kadhaa ndani ya eneo la Mikocheni huku akijifikiria mahala pa kwenda na hatimaye fikra zake zilimpa mahala pazuri pa kwenda.
Aliongoza gari na kuelekea kule alipokuwa akitaka kwenda kwa muda huo ili aweze kuanza kazi yake ya kumtafuta shemeji yake ambaye alikuwa amemfanya mpenzi wake kwa kiasi kikubwa asiwe na furaha kwa kutoweka kwake, safari yake hiyo iliishia jirani kabisa na Nyumba ya Waziri Kabaita baba yao Mzazi Annie na Andrew. Alisimamisha gari kwa mara moja akiwa anatazama usawa wa mlangoni kwa Waziri huyo, alikaa kwa muda wa dakika kadhaa akiwa hapo karibu lango la nyumba hiyo. Ukimya ndiyo ulikuwa umetawala nyumba hiyo na hakukuwa na dalili yoyote ya mtu kuwepo ndani ya eneo hilo, Moses hakutaka kabisa kuondoka katika eneo hilo kwa haraka sana yeye aliendelea kusubiri hapo  huku akiwa na shauku kubwa sana ya kupata kile alichokuwa akikitaka. Imani zake zilimuambia kabisa upoteaji wa Viktoria basi mmoja kati ya watoto wa familia ya Mzee Kabaita alikuwa akihusika na hilo suala ndiyo maana alianzia hapo nyumbani kwa waziri huyo ili kupata uhakika kile alichokuwa akikihisi ndani ya ubongo wake kama ni kweli. Hakuwa na mtu mwingine wa kumuwazia mabaya isipokuwa hao ndugu wawili wa damu ambao alitokea kuwachukia sana tangu mara ya kwanza walipoanza kumchefua ndani ya moyo wake.
Uadui wao katika penzi lake na Beatrice ndiyo ilikuwa ni sababu iliyomfanya aje kuweka kambi hapo kwa muda mfupi akichunguza kile kilichokuwa hapo, moyoni aliamini kabisa kuwa anaweza akawa ni Annie kamteka Victoria ili amushinikizee Beatrce aachane na yeye au ni Andrew kamteka Victoria ili ampate Beatrice kinguvu.

Alipozifikiria sababu hizo ndani ya kichwa chake hakuwa tayari kabisa kuondoka nyumbani kwa Waziri Kabaita, aliendelea kukaa hapo huku akiwa amefichwa na vioo vya giza vya gari aliyokuwa amekuja nayo asiweze kuonekana vizuri. Dhamira ya dhati ya kumpata dada wa mpenzi wake ili aione furaha ya mpenzi ndiyo ilikuwa imemtawala ndani ya moyo wake kwa muda huo wote aliokuwa hapo akisubiria huenda wawili kati ya hao.

Moyoni alikuwa na subira kuu katika kuwasubiri ndugu hao wawili waweze kutoka ndani ya nyumba yao ili aweze kuwafuatailia, alisubiri akiwa katika eneo hilo kwa kipindi cha muda na hatimaye subira yake ikazaa matunda baada ya kuona gari aina ya toyote verossa ya rangi nyeusi ikitoka ndani ya nyumba hiyo. Gari hiyo iliingia barabarani katika upande ambao gari la Moses lilikuwa limeegeshwa na kisha ikampita kwa kasi. Moses alisubiri hadi gari hilo lilipotokomea kabisa katika upeo wa macho yake ndiyo yeye akaingiza gari barabarani na kuanza kulifuatilia, alilifuatilia gari hilo kwa nyuma zaidi kwa mwendo wa kasi hadi alipofanikiwa kuliona gari hilo. Moses alipoliona alipunguza mwendo kidgo ili asiweze kulikaribia na aliendelea kulifuatilia gari hilo kwa karibu zaidi akiwa na lengo la kujua lilikuwa likielekea wapi. Bado hakuwa amejua kabisa kuwa aliyekuwemo ndani ya gari hilo alikuwa ni nani yeye aliamua tu kulifuatilia kwani kila mwana wa waziri Kabaita alikuwa na shaka naye sana na hakuwa tayari kumuacha yeyote atakayetoka ndani ya nyumba hiyo. Aliamini kabisa huyo aliyekuwa yupo ndni ya gari hakuwa Mzee Kbaita kwani kwa kipindi hiko alikuwa yupo bungeni Dodoma kwenye kikao cha bunge. Alilifuatilia gari hilo kwa umakini sana hadi lilipoingia kwenye barabara kuu ya magari yeye, gari hilo lilienda hadi katika mtaa wa pili kutoka ilipo nyumba ya waziri Kabaita, gari hiyo ilipofika mtaa huo iliingia katika nyumba yenye uzio mrefu na wenye nyaya, Moses alipoona gari hiyo imeingia mahala hapo aliamua kupitilia kwenye nyumba hiyo huku akiwa ameishika namba ya nyumba hiyo ambayo aliiona wazi kutokana na uwepo wa taa nyingi nje ya nyumba hiyo. Alipitiliza hadi mbele kidogo ya nyumba hiyo kisha akaliingiza gari kwenye sehemu ya maegesho ya magari ambayo hupenda kulaza magari kwa kulipa.
Hapo Moses alishuka ndani ya gari lake kisha akaandika jina katika kitabu cha wanaolaza magari, alilipa hela ingawa hakuwa akilaza gari kwa muda mrefu kisha akatoka eneo hilo na akaanza kutembea kwa miguu kurudi kule alipokuwa ametoka hapo awali.  Alipoikaribia nyumba ambayo ilikuwa imeingia hiyo gari alijifikiria kwa muda baada ya kumuona Mlinzi wa nyumba hiyo akiwa yupo Mlangoni katulia. aliamua kughairi kuendelea mbele baada ya kuona duka dogo la kuuza bidhaa rejareja likiwa lipo pembeni yake.
Hapo aliamua kuliendea duka hilo ambapo alipofikia alimkuta kijana wa makamo yake ndiyo muuzaji waduka hilo, hapo aliagiza sigara ingawa hakuwa mvutaji hata kidogo. Kwa pesa aliyokuwa nayo ilimbidi aagize pakiti zima la sigara ili aondoe usumbufu kwa Muuza duka, hela ya ziada iliyobaki alirudishiwa ambapo aliipokea ingawa haikuwa na ulazima nayo. Akili ya Moses ilimtuma kupokea pesa kwani laiti kama angeisamehe hiyo pesa ingekuwa ni kumpa wasiwasi  mwingine  Muuza duka na hata aanze kumfuatilia nyendo zake akiwa yupo katika eneo hilo, muonekano wake wa kujificha sura  kwa kofia pamoja na kusamehe hela iliyobakia alijua kabisa Muuza duka angepata furaha kwa kupata pesa hiyo na huenda hata angetaka kujua zaidi juu ya mtu huyo aliyetoa sadaka kwake na hapo ndiyo ingekuwa kuanza kumfuatilia kabisa.
Moses alipoiona sura ya kijana huyo wa makamo yake akiwa anauza duka aliamini kabisa kuwa haikuwa biashara yake bali alikuwa ameajiriwa ili aweze kupata mulo wa kila siku, hivyo angempa hiyo hela ingeenda kwenye mfuko wake moja kwa moja ndani ya muda huo na siyo katika hesabu ya duka hilo.



****


MUDA MFUPI ULIOPITA
Andrew baada ya kunywa shurubati ya maembe akiwa amekaa sebuleni kwao akitazama luninga alinyanyuka kwenye kiti akiiacha bilauri palepale mezani, alienda hadi zilipo funguo za magari ya hapo nyumbani kwao na alichukua mmojawapo wa gari hapo nyumbani kwao akawa anatoka kueleka kwenye mlango mkubwa ambao ungemuwezesha yeye kutoka nje ya nyumba hiyo. Alionekana alikuwa ni mwenye haraka sana huku akiwa haeleweki alikuwa anaelekea wapi ndani ya muda huo, alikuwa ni mwenye kukazana sana ili awahi huko mahali alipokuwa akitaka kuelekea kutokana na haraka aliyokuwa nayo.
"Wee Andrew!" Alisiikia sauti ya mama yake ikimuita ndani ya muda huo, ilimlazimu asimame na kugeuka nyuma ambapo alimuona mama yake akiwa anatokea sehemu vilipo vyumba vya kulala hapo nyumbani kwao.
"Unaenda sasa hivi Andrew mwanangu, una wiki ngapi baba hujafika shule hujui mitihani inakaribia hata ukae chini usome mwanangu" Mama alimlaumu.
"Mama nawahi mara moja mahali muhimu nitarudi" Andrew alijitetea
"Baba utamuaibisha baba yako ukifeli, ona dada yako huyo yupo chuo sasa hivi alipita huko hakufeli mwanangu" Mama yake aliendela kulaumu kwa sauti hadi Annie akatoka hadi mahali hapo walipo.
"Annie hebu mwambie mdogo wako aelewe ni muda wa kusoma huu siyo wa kuzurura" Mama alimuambia binti yake juu ya mwanae wa kiume na hakujua kabisa kuwa watoto wake hao walikuwa ni chui na paka hawapikiki chungu kimoja kabisa.
"Mama huyo mkubwa mzima sasa hadi alipo anajielewa vilivyo ukisema upige kelele haitasaidia kitu, na wewe  dogo mheshimu mama ukae utulie" Annie alijifanya kumfokea Andrew ingwa alijua kufokea huko hakutasaidia chochote mbele ya adui yake huyo.
"Bora Annie mwanangu ukae umuambie mdogo wako naona mimi hanielewi kabisa mtoto huyu au kwasababu baba yake hayupo kwa muda mrefu ndiyo anatawala nyumba hii hadi anashindana na mimi kimaamuzi" Mama Annie kulalamika.
"Mama ya nini kuumiza kichwa na huyu hadi uwe hivyo si mwenyewe anajitambua kuwa anahitajika shule wewe ni kumkumbusha tu, akipinga amri zako jua hana adabu" Annie aliongea huku akimtazama Andrew ambaye tayari alikuwa ameshakunja macho yake kwa hasira aliposikia maneno hayo.
"Ngoja mimi nikampumzike tu ndani maana kichwa kinaniuma kwa jambo moja hilohilo kila siku" Mama Annie aliongea kisha akarudi chumbani kwake akiwaacha wanae wakiwa wamekaa peke yako sebuleni, hakujua kuwa kama wakibaki wenyeewe wanao hao kunakuwa hakuna mapatano kabisa baina yao yeye  aliona ndiyo wanaopatana na watakaa washauriane mambo mbalimbali. Alipofika chumbani kwake na kufunga tu mlango wa chumba chake  alikuwa ameacha kitu kingine tofauti na aliyokuwa akifikiria juu ya watoto wake, sauti ya kufunga kwa mlango wa chumbani kwake iliposikika tu wote walitazamana kwa sura zilizojaa chuki kuu wakiwa wapo pamoja mahala hapo.
"Unajifanya muongeaji sana siyo?" Andrew alimuuliza dada yake kwa hasira
"Ndiyo we unaamua nini? We bwege angalia sana mama yangu akija kufa kwa presha kisa ujinga wako sitakuacha mzima wewe" Anie naye alikoroma.
"Hebu nitolee upuuzi wako na nakuambia nikija kukutia nguvuni wewe nakufanya chakula tu"
"Thubutuu! Nikikushika wewe unakuwa mke wa vijana wangu, tena ukijaribu kuingia tu kwenye anga zangu jua Victoria namchinja na kisha namuambia Beatrice umemuua wewe halafu namfuata Beatrice mwenyewe namchinja pia"
"Ukijaribu lolote kati ya hayo ndiyo kiama cha bwege wako yule unayemuita kipenzi cha moyo wako nakuambia, nitamkatakata Moses vipandevipande nakuambia"
"Kajaribu uone, mimi sikuambii chochote ila ingia kwenye anga zangu utaikuta maiti ya Beatrice asubuhi inayofuata. Hayawani wewe" Anni alipoongea  maneno hayo aliondoka moja kwa moja na kurudi chumbani kwake akimuacha mdogo wake akiwa amesimama kwa hasira akiwa ameshika funguo za gari.
Andrew alisimama hapo akiwa ameghadhibika sana kwa maneno aliyokuwa ameambiwa na dada yake ambaye kwa muda huo hakuwa ana muhesabia ni dada, ndiyo maana alikuwa yupo radhi hata kumbaka akimteka ili amalize hasira zake kisha amuue. Hakika kutetea mapenzi yao na kupendwa wasipopenda ndiyo kuliwafanya ndugu hawa hadi wawe namna hiyo kwa kipindi hiko, walikuwa wakipendana sana lakini ujio wa Moses na Beatrice katika maisha yao ndiyo sababu pekee iliyowafanya wawe maadui. Kipindi cha nyuma cha mapenzi yao kama kaka na dada tayari walikuwa wameshakisahau na sasa muda huo walikuwa wakichukuliana kama maadui wawili waliokuwa hawapo tayari kuwa pamoja hata kwa namna gani. Aliganda hapohapo kwa dakika takribani mbili ndiyo akaamua kutoka nje ya nyumba yao na kuondoka, alitumia gari aina ya Toyota Verossa na ndiyo iliyotoka nje ya geti la nyumba yao Moes akaifuatilia akiwa na anataka kumpeleleza zaidi.
 Alikuwa tayari amemkosa yule ambaye alikuwa ni mhusika mkuu wa kupotea kwa Shemeji yake na akawa anamfuata mtu ambaye hakuwa na kuhusika kokote na kupotea huko kwa shemeji yake. Mtu huyo aliyekuwa akimfuata alikuwa ndiyo adui yake nambari moja ambaye mwenyewe hakuwa amemjua kama ndiye huyo, adui huyo ambaye kamaa angefanikiwa kumtia nguvuni basi angemmaliza mara moja na si kama adui yake wa pili ambaye alikuwa akimtaka awe hai kwa namna yoyote ile.


****


Moses akiwa na pakiti la sigara mkononi mwake ambapo hakuwahi kuvuta sigara ila siku hiyo ilimbidi awe hivyo, alipita jirani kabisa na geti la nyumba ambayo gari la Andrew ilikuwa limeingia. Ilikuwa ni ndani ya nyumba ya Komredi ambayo Moses hakuwa anaijua kabisa kuwa nyumba hiyo ilikuwa ni ya mhalifu hatari sana,pembeni ya geti la nyumba hiyo alikuwa amekaa mtu ambaye alikuwa ana mwili uliojengeka kimazoezi akiwa ameshika sigara ambayo ilkuwaa ipo nusu akiwa anaivuta taratibu sana. Moses alimsogelea mtu huyo kisha akasimama mbele yake, alimtazama kwa namna ambayo mtu huyo hakuweza kabisa kuitambua sura yake ambapo mtu yule alitoa sigara mdomoni mwake akabaki anamtazama Moses huku akipapasa mkono kiunoni mwake. Jambo hilo Moses aliliona lakini hakutaka kabisa kuwa na papara yeye alijifanya kama hajauona huo mkono wa mtu huyo kiunoni, alichukua sigara kwenye pakiti kisha kwa namna ya kuonekana alikuwa ni mzoefu wa mambo hayo alimuoneshea huyo mtu sigara.
"Moto babu nitoe kiu" Moses alimuambia huyo jamaa
"Aaaah! Kumbe hiko tu aina noma mtu wangu sema usijinie kama mvamizi si unajua nipo lindo" Naye alimuambia Moses huku akimpatia sigara yake, Moses aliichukua sigara hiyo kisha akaweka sigara yake mdomoni na akagusanisha na sigara hiyo hadi ikawaka.
"Hapa mambo mwake kabisa nina mzuka nazo nayo fegi kinyama toka waniachie" Moses aliongea huku akivuta sigara hiyo.
"Vipi man ulikuwa gizani(gerezani)?" Jamaa aliuliza
"Acha mtu wangu mwaka wa tano huu ndiyo natoka leo yaani hapa sina hata mchongo wa kuniweka town"
"Dah! Ebwanaeh! Masala gani ulikuweka ndani?"
"Nilitia mtu mabeto(mpanga) nusu ya kuua si unajua dili zangu zilikuwa hizo town mtu ananilipa nimfanyie mwingine"
"Duh! Man sasa tupo harakati moja na bosi wetu ni mtu wahrakati hizohizo man, kama umewahi kumsikia Komredi hapa ni nyumbani kwake kuhusu mchongo tu utapata we njoo tumoro tu"
"Haina mbaya kama dili za kupasua watu na mabeto nipo  gado tu hata nyingine tu"
"Man zipo dii kibao humu hata kutafuta wateja sana tu maana ndani kuna madem wa kunyonga(machangudoa) wengi sana"
"Haina kwere mwanangu wacha niwahi kwa msela si unajua kanihifadhi usiku huu tu kesho nazuka hapo"
Wote kwa pamoja waligongesha mikono yao kwa ishara ya kuagana wakiwa wamekuwa na urafiki kwa muda mfupi tu,Mlinzi wa pale nyumbani kwa  Komerdi yeye aliona alikuwa amepata rafiki lakini kwa Moses alikuwa anshukuru sana kwa kuweza kuwa karibu sana na huyo mtu na aliona nafasi pekee ya kuweza kuingia ndani ya nyumba hiyo ilikuwa ndiyo hiyo hapo. Aliposikia habari ya uwepo wa machangudoa ndani ya nyumba hiyo aliona kabisa kuwa kuna uwezekano wa kuwepo Shemeji yake humo ndani, kiupande alihisi kuwa anaweza kuwa amekamatwa ili aende kuuzwa kama wanawake wengine ili aweze kumkomoa Shemeji yake.


Baada ya kutoka katika eneo hilo hakuwa na mahala pengine pa kwenda zaidi ya kwenda kuzunguka katika mtaa mwingine kama mzururaji, alizunguka katika kila mitaa na hatimaye akarudi kule kwenye mtaa aabao alikuwa ameegesha gari lake. Hapo alisaini kitabu kuwa ameshachukua gari na aliamua kuondoka huku akiwa amejipongeza kwa hatua nzuri aliyokuwa amefikia ndani ya siku hiyo tangu aanze kazi yake hiyo hatari. Uhatari wa kazi hiyo hakuwa ameuona kabisa alichojalia yeye ilikuwa ni kurudi kwa furaha ya mpenzi wake na si vinginevyo, mapenzi huondoa hofu kabisa ya kutetea penzi ndiyo maana Moses hakuwa na hofu kabisa kutetea penzi lake liwe na furaha kwa namna yeyote ile.


*MOSES AISOGELEA NGOME YA JOMREDI NA GOTTA(ANDREW)
 


ITAENDELEA!!








MWENYE KUIHITAJI RIWAYA HII HADI MWISHO ANAWEZA KUWASILIANA NA MTUNZI KUPITIA NAMBA ZAKE HAPO JUU KWA NJIA YA UJUMBE MFUPI TU WA MANENO NA SI KUPIGA. HUKO UTAIPATA YOTE.



KWA RIWAYA ZAIDI LIKE UKURASA WETU WA FACEBOOK AMBAO NI:





No comments:

Post a Comment