Thursday, January 19, 2017

WAKALA WA GIZA SEHEMU YA AROBAINI NA MOJA



RIWAYA: WAKALA WA GIZA

MTUNZI: HASSAN O MAMBOSASA


SIMU: +255713776843
          +255762219759


WHATSAPP: +255713776843

SHUKRANI ZOTE ANASTAHIKI MWENYEZIMUNGU MUUMBA WA ULIMWENGU WOTE KWA KUNIWEZESHA KUANDIKA RIWAYA HII NIKIWA NA AFYA NJEMA




______________+18__________________




SEHEMU YA AROBBAINI NA MOJA!!

   Alipoiona kamera hiyo alitoka moja kwa moja ndani ya wodi hiyo kwa haraka sana akaeleka mapokezi katika hospitali hiyo, alitumia dakika mbili kutoka wodi aliyokuwa amelazwa Mufti hadi mapokezi akawa amefika kutokana na umbali uliopo.
 
   Alipofika hapo mapokezi DCP John akiwa yupo ndani ya mavazi ya kiraia alitoa kitambulisho cha kazi na akajitambulisha halafu akasema, "nahitaji kuonana na mhusika wa chumba cha kuongozea CCTV kamera sasa hivi"





________TIRIRIKA NAYO

                   “Sawa afande subiri  niwape taarifa” Msichana aliyekuwa mapokezzi aliongea
 

                 “what?! Hebu nyanyuka hapo na unipeleke haraka sana kwani hawajui uwepo wa askari eneo hili” DCP John alimjia juu Msichana huyo aliyekuwa amevaa mavazi ya kiuguzi
 
                   “Lakini ndiyo utaratibu wetu jamani” Muuguzi huyo aliongea kujitetea
 
                  “Binti hebu nitolee upuuzi unajua nipo kazini hapa, toka uongoze njia unanipotezea muda kama mtuhumiwa yupo ndani ya hiii ya hospitali si atatoroka hadi muda huo!”
 
                  “Lakini..”
 
             “Shut up usinifundishe kazi eti nisubiri nasema toka hapo kwenye desk la receiption uniongoze kabla sijamuita Daktari mkuu wa hii wa hospitali, unampangia Kamishna msaidizi kazi ya kufanya binti siyo. Sirudii tena kukuambia nauliza hivi tunaenda au hatuendi?”
 
                    “Sawa nakupeleka”
 
                   “Haya ongoza njia haraka sana”
 
   Yule Muuguzi hakuleta pingamizi zaidi aliamua kumpeleka DCP John kule alipokuwa akitakiwa kwenda kwa muda huo akaendelee na uchunguzi wake juu ya balaa lililomtokea hapo hospitalini, tayari alikuwa anajua alikuwa amemtibua DCP John kwa muda huo ndiyo maana alikubali mwenyewe kufuata  kile alichokuwa akikitaka kwa muda huo. Mawazo yake DCP John alikuwa ni polisi wa kawaida ndiyo maana hata alifikia hatua ya kujifanya anamuelewesha pale alipokuwa amempa amri, kujitambulisha kwa DCP John bila kumtajia cheo chake ndiyo jambo ambalo lilimfanya aamini DCP John alikuwa ni askari wa kawada tu hata alipomuonesha kitambulisho kilichokuwa kimekamilika kimaelezo hakuwa na muda wa kukikagua kabisa aliamini alikuwa akiongea na askari wa kawaida tu. Hata alipotajiwa cheo baada ya kuwa amemkasirisha bado hakuwa akiamini kutokana na umri aliokuwa nao DCP John kuwa na cheo hicho, alizoea kuona Makamishna na makamishna wasaidizi wa jeshi la polisi wakiwa ni watu wazima si kama alivyokuwa akimuona DCP John kwa muda huo. 
 
    Walipokuwa wakielekea hicho chumba chenye mitambo ya kuongozea kamera ndiyo walianza kuamini kuwa kile kilichokuwa kikielezwa na DCP John ilikuwa ni kweli tupu kwani maaskari kila alipokuwa wakipita walikuwa wakimpigia saluti DCP John hata wale waliokuwa na nyota mabegani mwao jambo ambalo lilimfanya Muuguzi huyo azidi kuwa na hofu kwa kujifanya muongeaji sana  na hata kitambulisho cha  DCP John kutokitazma kwa ufasaha. Alikuwa akimpeleka DCP John huku akiwa na hofu ndani ya moyo wake kutokana na hasira alizokuwa amemuonesha pale mapokezi wakati akimuambia kuhusu jambo hilo, baada ya muda wa dakika kadhaa walikuwa tayari wameshafika kwenye mlango wa chumba cha kuongozea kamera ambao ulikuwa na kengele maalum mlangoni. Muuguzi huyo aliibonyeza kengele hiyo na haikupita muda mlango wa chumba hicho ulifunguliwa, alitoka kijana aliyekuwa amevaa mavazi ya walinzi wa hospitali hiyo ambapo alitoa tabasamu tu alipomuona DCP John katika eneo hilo.
 
                      “Karibu Afande” Kijana huyo alimkaribisha
 
                     “Asante, nahitaji kulijua jina lako “ DCP John aliiitikia ukaribisho kasha akaomba kulijua jina la huyo kijana aliyemkaribisha katika eneo hillo, muda huohuo Yule Muuguzi baada ya kumfikisha katika eneo hilo alianza kuondoka akijua tayari yalikuwa yameshaisha.
 
                  “Wee! Unakwenda wapi bado hayajakwisha haya, leo hii mpaka kwenye uongozi wa hospitali hii ndiyo yatakuwa yameisha subiri hapa” DCP John alimuambia Muuuguzi huyo ambaye alizidi kuingiwa na hofu zaidi
 
                       “Afande naitwa Godwin ndiyo  mhusika mkuu wa chumba hiki cha kuongezea kamera katika hospitali hii, vipi afande huyu dada yetu kakufanyaje?” Kijana huyo alijitambulisha kisha akauliza kuhusu huyo muuguzi ambaye hadi muda huo tayari machozi yalianza kumlenga akifikiria kupelekwa kwenye uongozi wa juu wa hospitali hiyo.
 
                  “Huyu hana adabu anachelewesha kazi, atasubiri hapa mpaka tutoke humo ndani nitakapomalizana na wewe. Tunaweza kuingia ndani nahitaji kujua kila kitu kilichokuwa kikiendelea kabla ya tukio hili” DCP John aliongea na Godwin alikubali kuingia naye ndani huku Yule Muuguzi akiwa amebaki mlangoni akiwa na uoga wa kupoteza kibarua chake mbele ya Askari ambaye aliamini kabisa alikuwa na jazba ya kucheleweshwa kile alichokuwa akikihitaji. Binti Yule aliendelea kusubiri pale akijua kuwa kazi ilikuwa imeisha lakini baada ya dakika moja tu DCP John alitoka nje akamkuta binti huyo tayari machozi yalikuwa yanamtoka kwa kuhofia kupoteza kibarua chake, alipomuona DCP John alimtazama kwa huruma sana akitarajia huruma hiyo itaweza kumshawishi DCP John  aweze kumsamehe asimpeleke kule alipokuwa akitarajia kumpelekea kwa muda ambao atakuwa tayari ameshamalizana na  kijana wa chumba cha kuongozea kamera.
 
                             “Binti” DCP John aliongea alipotoka nje ya chumba hicho huku akimtazama Yule Muuguzi ambaye alinyanyua kichwa chake akamtazama DCP John aliposikia kuiitwa kwake na afisa huyo wa ngazi ya juu katika jeshi la polisi.
 
                          “Nenda mapokezi binti kutokea kwa tukio hili si kwamba huduma za hospitali zimesimama kumbuka kuna mamia ya  wagonjwa wanawasili ndani ya hospitali hii mapokezi panahitaji mtu” DCP John alimuambia.
 
                                 “Afande nisamehe niko chini ya miguu yako” Muuguzi huyo aliongea huku akilia akijaribu kumpigia magoti DCP John lakini alizuiwa.
 
                               “Haina haja binti mimi kaendelee na kazi ila nidhamu uwe nayo unapokuwa kazini binti na uendane na mazingira yalivyo si kujifanya unajua kila kitu kuhusu kazi ya mtu, nikiharibu kazi lawama pia kwangu” DCP  John aliongea kwa upole tofauti na alivyokuwa na ukali kama alivyokuwa akiongea hapo awali alipofika kwenye mapokezi ya hospitali hiyo, Muuguzi alionekana kutoamini kutokana na imani aliyokuwa nayo juu ya polisi wakiwa  wana hasira kuwa ni watu ambao kusamehe ni ngumu sana. Alibaki akiwa ana mshangao asiamini kile alichokuwa ameambiwa na DCP John kwa muda huo na hata tabasamu hafifu lilianza kuonekana katika uso wake alipoambiwa maneno hayo, alimshangaa tu DCP John kwa maneno yake aliyokuwa ameyaongea ndani ya muda ambao alikuwa akitarajia kufukuzwa kazi yake aliyokuwa akiitegemea.
 
                           “Nidhamu ni muhimu binti izingatie sana, siwezi kukufanya ufukuzwe kazi kwakuwa najua ndiyo msingi wako wa maisha hivyo usiwafanye wengine wakaharibu kazi zao kwa kufanya kazi vile ulivyokuwa ukitaka wewe ni mbaya sana hiyo kwani wana hofu ya kuharibiwa kazi kama ulivyokuwa nayo wewe. Unangoja nini nenda sasa ukaendelee na kazi au nikupeleke uongozi wa juu kwa kukaa hapa huko mapokezi hamna mtu” DCP John aliongea maneno  hayo huku akimtazama Muuuguzi huyo kwa uso wa upole sana, Muuguzi huyo bado hakuwa ameondoka alibaki akimshangaa Dcp John. DCP John  aliamua kumkazia macho na kumpa mkwara wa kimsihara ambao ulifanya Muuguzi huyo wa kike atabasamu kisha akageuka akimuacha DCP John naye akiwa anatabasamu kisha akasikitika baada ya Muuguzi huyo kuanza kuondoka, baada ya Muuguzi huyo kuondoka DCP John aliingia ndani ya chumba cha kuongozea kamera kwa mara nyingine.



****

    MUDA MFUPI KABLA
  Hata kabla hotuba mkutano na waandishi wa habari na Mufti haujaanza ndani ya hospitali ya Aga Khan tayari Josephine alikuwa ameshawasili ndani ya hospitali hiyo akiwa na kitambulisho cha wauguzi wa hospitali hiyo, aliingia hadi ndani kabisa katika vyumba vya wauguzi wa hoospitali hiyo na akabadili nguo alizokuja nazo akavaa nguo nguo za wauguzi wa hospitali hiyo  ambapo katika sare yake hiyo alivaa ni mfumo wa suruali ambayo ilifanya umbo lake lionekane vyema na hata aliivaa hiyo ili aweze kuwa na wasaa mzuri wa kufanya kazi ambayo ilikuwa imemleta mahali hapo. Kichwani alikuwa amevaa wigi ambalo lilikuwa limembadilisha kabisa na asitambulike kwa urahisi na mtu yeyote aliyekuwa akifahamiana  naye kama akikutana naye katika maeneo hayo, usoni alikuwa amevaa miwani ya plastiki ambayo haikuwa na tofauti kabisa na miwani za wenye matatizo ya macho ambayo ilimfanya azidi kuonekana na muonekano tofauti kabisa. 

   Baada ya kuvaa hivyo Josephine hakucheza mbali kabisa na maeneo ya karibu na wodi ambayo alikuwa amelazwa Mufti akiwa na lengo moja tu la kumuangamiza Mufti  ikiwa atatoa siri za mpango wao uliokuwa upo mbioni kutimia, alikaa katika eneo hilo akiwa yupo tayari kukabiliana na hali yoyote itakayokuwa imejitokeza katika eneo hilo la hospitali kwa muda huo ilimradi tu Mufti aende kaburini akiwa ametoa siri za mpango wao uliokuwa unampa ulaji. Muda ambao waandishi wa habari walikuwa wakiingia ndani ya hospitali hiyo kwa lengo la kuitikia wito wa Mufti wa kuzungumza nao kwa jioni hiyo, tayari alikuwa ameshajisogeza jirani kabisa na wodi hiyo lakini kutokana na watu waliokuwa wapo humo ndani alikosa kabisa nafasi ya kumuua Mufti. Alikaa kwenye kundi la wauguzi ambao waliokuwa wamesogea karibu na wodi hiyo kusikiliza kile ambacho alikuwa akikiongelea Mufti, uwepo wa waandishi wa habari uliwavuta zaidi wauguzi wa hospitali hiyo kusikiliza kile alichokuwa akikiongea Mufti kwa muda huo aliokuwa amewaita hapo. Wauguzi hao walijazana mahala hapo ndiyo walikuwa wametoa kichaka kizuri ambacho kilimvutia huyo malikia wa chui(Leopard Queen) kama alivyokuwa akijiita akiwa katika kazi hizo, wakati waandishi wa habari wakitayarisha kamera zao kawa ajili ya kufanya mahojiano na Mufti yeye  alikuwa akifikiria tu namna ya kupenya katika kundi la watu hao na kumuua Mufti pasipo kugundulika na mtu yeyote aliyekuwa yupo katika eneo hilo. Akiwa anayafikiria masuala hayo simu yake iliingia ujumbe mfupi wa maneno ambao ulimfanya kusogea pembeni na kuusoma ujumbe huo, hakuwa tayari kuusoma ujumbe huo akiwa katikati ya kundi la wauguzi hao wa kike kwani alikuwa akitambua kabisa tabia ya wanawake ya kutia jicho katika mahali ambapo palikuwa hapawahusu hivyo alihofia kujikaanga mapema kwa mafuta ya mwili wake mwenyewe mithili ya kondoo.

               "Shosti shem nini huyo" Mmoja wa wauguzi alimuuliza akijua ni mwenzao katika hospitali hiyo, Josephine alimtazama kisha akaachia tabasamu jambo ambalo lilifanya kundi hilo la wauguzi kumcheka kimyakimya wakijua alikuwa amewakimbia ili kuwasiliana na mpenzi wake na aliogopa kuwasiliana naye akiwa yupo katikati yao.

            "Hapana chezea mzee wewe utaenda kujificha mwenyewe uchat naye" Muuguzi mwingine alidakia kwa sauti ya wastani huku akiusindikiza mzigo wa Josephine uliokuwa ukileta fujo alipokuwa akiwahi kwenda kujibu ujumbe mfupi ambao ulikuwa umeingia kwenye simu ambao alikuwa akiamini kabisa ulikuwa ukitoka kwa Wilson.

   Alipofika kwenye kona moja ya kumbi nyembamba(korido) za hospitali hiyo kusipokuwa na mtu aliitoa simu hiyo na kuusoma ujumbe ambao ulikuwa umeandikwa, 'tayari nipo ndani nimevaa kofia ya cowboy nimebeba kamera kubwa ya kizamani Mufti ni asusa yangu ikiwa atatoa siri hivyo niachie mimi huyo'

   Alipomaliza kuusoma ujumbe huo alitoa tabasamu hafifu kisha akaifunga simu yake ya kisasa kwa kubonyeza kitufe cha kuzima mara moja na kupelekea mchoro wa siri ujiweke kwenye kioo cha simu hiyo, baada ya hapo alirudi kule alipokuwa amekaa na wauguzi wenzake akatulia akiwa kama msikilizaji wa kile alichokuwa anataka kukiongea Mufti. Maneno ya Mufti yalipoanza alitulia kimya akiwa anasikiliza kile kilichokuwa kikitarajiwa kuzngumzwa na Mufti baada ya kuamka huko, kundi la wauguzi wenzake walikuwa wakidhani kuwa Mufti alikuwa akieleza kukumbwa na balaa lililomfanya apoteze fahamu. Walikuwa wakitarajia angezidi kuwaumbua wabaya wake ambao alikuwa amewataja hapo awalina kuwashutumu kuwa ndiyo chanzo cha kifo hiko, alipoanza kuongea walivumilia na kumsikiliza  hata kwa maneno ya lugha ya kiarabu aliyokuwa akiyatumia kwenye utangulizi wa hotuba yake hadi akaingia kwenye maneno ya lugha ya kiswahili. Alipoanza kukiri uovu wake wengi wa  wauguzi hao waliweka viganja vya mikono yao kwenye vichwa vyao kwa kutoamini walipokuwa wakisikia maneno hayo, walijuta  hata kumpa huduma mtu kama huyo aliyekuwa akifanya mambo mabaya kama hayo ambayo alikuwa ameyakiri mwenyewe mbele ya vyombo vya habari. Maneno hayo yalipofikia hapo simu ya Josephine iliita ambapo ilimlazimu anyanyke aende kwenye eneo alilokuwa awali wakati anaenda kusoma ujumbe mfupi wa maneno ulioingia kwenye simu yake, alipofika kwenye eneo hlo aliipokea simu yake kisha akatoa kitambaa akakiweka jirani na mdomo wake.

            "Ndiyo mheshimiwa.....ndiyo tupo ndani ya hospitali....sawa mheshimiwa ngoja nimuambie Wilson aliyekuwa ndani.....sawa"Simu ilikatwa na Josephine alifungua sehemu ya majina kwenye simu yake akaitafuta namba ya Wilson kisha akaipiga na akaiweka simu sikioni kuisikiliza ilivyokuwa ikiunganisha hadi ilipoaanza kuita.

         "Maliza kazi  Mheshimiwa kashacharuka" Aliongea baada ya simu kupokelewa kisha akakata simu baada ya kumaliza kuongea na akairudisha simu kwenye mfuko wa suruali yake ya kitabibu, alirudi katika eneo alilokuwa amekaa hapo awali pamoja na wauguzi wengine wa hospitali hiyo


<><><><><><><><><><><><>><><>

   Baada ya Wilson kupigiwa simu na Josephine ilikuwa inamsihi amalize kazi iliyokuwa imemleta ndani ya eneo hilo, alishikilia kamera ya kubwa na ya kizamani aliyokuwa amekuja nayo humo ndani kisha akaweka jicho sehemu ya kuweka jicho wakati anachukua mkanda. Alikuwa amebeba kamera ambayo yalikuwa yakitumika kipindi cha nyuma sana kwenye baadhi ya vituo vya televisheni nchini, alipokuwa ameweka jicho ndani ya kamera hiyo kila mtu aliyekuwa yupo karibu yake alidhania alikuwa akichukua mkanda wa video kwa ufasaha katika kamera hiyo ambayo ilikuwa imewekwa kwenye misimamio(stand) yake. Jambo ambalo hawakutambua ni kuwa ndani ya kamea hiyo kulikuwa na mashine kweli ya kuchukua mkanda lakini pia kulikuwa na silaha inayotumia risasi ndogo kama bastola za kawaida, tundu la kutolea risasi hiyo lilikuwa lipo juu ya lensi ya kamera hiyo na muda huo aliokuwa akiweka chini kwenye kamera hiyo alikuwa akimlenga Mufti kwa kutumia silaha hiyo. Baada ya kuhakikisha kuwa Mufti alikuwa yupo kwenye usawa wa tundu la risasi alishikilia mshikio ambao ulikuwa upo chini ya kamera hiyo, aliuvuta mshikio huo kwa taratibu na risasi ilitoka na ikaenda kumpata Mufti kwenye kifuo chake moja kwa moja.  Ulipokuwa ukitokea mparanyiko wa watu wakijua wamevamiwa ili wanusuru maisha yao yeye  aliichomoa kamera yake kwenye kisimamio na kuutoa waya wa kipaza sauti kwa haraka na kuushika mkanda wa kuivaa  begani akaivaa kisha akajichanganya na waandishi wa habari wengine kukimbia kuelekea nje ya hospitali hiyo. Alifanikiwa kutoka nje ya hospitali bila kutiliwa shaka lakini alipokuwa huko nje alipokuwa akielekea ndiyo shaka ilikuwa zaidi.

   Kitenda cha kutoka nje ya hospitali hiyo akijifanya anakimbia kuokoa maisha yake hakujua kabisa muonekano wake ulikuwa umeshamtia shaka Norbert ambaye tayari alikuwa ameshafika katika hospitali hiyo tangu Mufti akiwa anaaanza kutoa maelezo yale. Norbert hakuwa ameingia ndani ya hospitali hiyo bado alikuwa yupo nje ya hadi Mufti alipopigwa na risasi, taarifa za kupigwa risasi kwa Mufti alikuwa ameshazipata kutoka kwa Eva ambaye alikuwa yupo ndani. Wilson alipotoka akiwa katika muonekano wake wa kiutuzima pamoja na kamera yake kubwa ambayo hakuwa ameiacha, hapo ndipo Norbert alikuwa amemtilia shaka na alianza kumfuatilia shaka Wilson ambaye bado hakumjua kama alikuwa ni Wilson huyo. Wilson alionekana kukimbia mbio sana lakini Norbert naye akiwa amevaa kofia  iliyokuwa imeufunika uso wake alikuwa akitimua mbio sawa na yeye na alikuwa anamfuatilia kwa  kasi ya kawaida. Wilson alikuwa akikimbia kwa kasi huku akiishikilia kamera yake isiweze kuanguka , alikuwa akiifuata barabara ya Sea view baada ya kuyavuka  makutano ya barabara ya Obama, Sea view na barabara ya Ufukoni. Hakuwa akiangalia nyuma kabisa yeye alikuwa akitimua mbio hadi alipofika kwenye shule ya msingi Almutazir iliyopo pembezoni mwa barabara ya Sea view ndiyo akakumbuka kuangalia nyuma kuona kama alikuwa anafuatiliwa, alipoangalia nyuma hakubahatika kumuona yeyote aliyekuwa akimfuatilia kwani Norbert alishawahi kujibana kwenye mti uliopo pembezoni mwa barabara. Hapo Wilson aliendelea kukimbia kama kawaida akiwa anaivuka shule ya msingi Almutazir hadi akafika mbele kidogo ambapo alivua kofia aliyokuwa amevaa akaitupa kisha akangalia tena nyuma, Norbert aliwahi kubana kwa mara nyingine kwenye gari ambalo lilikuwa limeegeshwa pembezoni mwa barabara. Wilson alipoona haoni mtu alivuka barabara akawa anaelekea ufukweni akiwa yupo huru kabisa akijua kuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa akimfuatilia kwa muda huo, alipovuka barabara alikuwa yupo karibu kabisa na ufukwe wa bahari katika eneo lenye mwanga hafifu kabisa  pamoja na nyasi fupi zilizopo mita kadhaa kutoka ulipo mchanga wa ufukweni mwa bahari. Norbert alikaza mwendo katika kumsogelea Wilson pasipo yeye mwenyewe kujua kama alikuwa akisogelewa na mtu kama huyo mwenye kila aina ya hatari akiwa yupo katik kazi yake hiyo ya upelelezi, Norbert alimpofika kabisa Wilson kwa nyuma alimshika begani kisha akaavua kofia. Wilson aligeuka kwa haraka baada ya kushikwa begani na Norbert na kwa msaada wa mwangaza hafifu wa eneo hilo aliweza kumtambua kabisa alikuwa ni Norbert huyo aliyekuwa amemgusa begani, Norbert pia aliweza kutambua kuwa aliyekuwa ametoka ndani ya hospitali ile akiwa kama mwandishhi wa habari alikuwa ni Wilson ambaye ndiyo yupo mbele yake kwa  hatua tatu tu.

           "Oooh!" Damn!" Wilson aliongea kwa mshangao uliochangayika na hofu baada ya kumuona Norbert maeneo hayo katika muda ambao hakutarajia kukutana naye tena akiwa peke yake bila ya kuwa na wenzake kama alivyokuwa akikutana naye hapo awali, aliona hatari kubwa ilikuwa ipo mbele yake ila hakutaka kujileta kijinga mbele ya mtu hatari kama huyo ambaye yupo kazini kuhakikisha mpango wao unaharibika, kitendo cha haraka alichokifanya Wilson baada  ya hapo ilikuwa ni kumrushia Norbert kamera yake ambayo ndani ilikuwa na silaha ambayo ilitumika kumfanya Mufti asiendelee kuwaharibia mipango yao mbele ya watanzania. Kamera hiyo nzito aliirusha usoni mwa Norbert ambaye alihama pembeni haraka sana ikapita ikaanguka chini, kitendo cha Norbert kuhama pembeni ndiyo Wlson aliitumia kama nafasi ya kugeuka nyuma na kuanza kukimbia kwa nguvu zake zote ili amuepuke Norbert. Alikuwa akitambua wazi kabisa hawezi kupambana na mtu kama huyo ambaye uhatari wake alikuwa ameshauona kupitia habari alizosikia juu  yake hasa kutangulia mbele za haki kwa wenzake na chanzo kikubwa ikiwa ni Norbert.

 Norbert naye hakutaka kumuachia kabisa Wilson amtoroke kijinga namna hiyo, aliamua kumkimbiza kwa nguvu zake zote ambapo tayari muda huo Wilson alikuwa ameshaelekea kwenye mchanga wa ufukweni akawa anakimbia kuufuata upande wa kaskazini ambao kulikuwa na kampuni ya Tanzania Safaris Zanzibar Travel holidays. Norbert alimkimbiza kwa nguvu zote  na akawa anatumia kasi yake aliyokuwa akiitumia kipindi yupo kwenye mafunzo ya hatari kabisa ambayo alikuwa akipewa nchini Cuba baada tu ya kuchukuliwa na EASA kwa mara ya kwanza, haikumuwia muda mwingi kwa kutumia kasi hiyo kwani tayari alikuwa ameshamfikia Wilson na akawa yupo naye karibu kabisa akiwa yupo katika kasi sawa naye baada ya kupunguza kasi alipomfikia karibu naye. Wilson alikuwa akitumia nguvu zaidi katika kukimbia huku akiwa amebana mdomo kwa nguvu sana  asiweze kuvuta pumzi kwa kutumia mdomo, akiwa bado yupo kwenye mbio na kasi yake hiyo Norbert aliupiga teke dhaifu mguu wake mmoja na kupelekea ugongane na mguu mwingine kisha aanguke vibaya na kubiringita kwenye mchanga.

                "Aaaah!" Alitoa sauti ya kukata tamaa kwa kuangushwa na Norbert huku akiwa anasalimiana na mchanga huo wa ufukweni.




*WAZIRI MMOJA AAAGIZA MUFTI AUAWE, NI  NANI HUYO?

*WILSON USO KWA USO NA MZEE WA FAGIO

*JOSEPHINE KUBAKIA HOSPIITALI WAKATI MUFTI  BADO ANAPUMUA

*DCP JOHN KAZINI


SEHEMU YA AROBAINI NA MOJA SI MBALI SANA USIIKOSE KUJUA HATMA YA MAADUI WA TAIFA MBELE YA MZEE WA FAGIO




No comments:

Post a Comment