Wednesday, September 2, 2015

DHAHAMA


 RIWAYA: DHAHAMA


MTUNZI: HASSAN O MAMBOSASA


SIMU:+255713776843
+255762219759

WHATSAPP:+255713776843


SHUKRANI ZOTE ANASTAHIKI MWENYEZIMUNGU
MUUMBA WA DUNIA NA VILIVYOMO KWA KUNIPATIA
AFYA NJEMA ILIYONIWEZESHA KUANDIKA RIWAYA
HII KWA MARA NYINGINE



 SEHEMU YA KWANZA!!


SURA YA KWANZA
    Hali ya simanzi ilikuwa imetawala katika eneo zima la kasri la kupendeza la kifalme katika himaya ya Majichungu inayopatikana katika bahari ya hindi, himaya hii ya kijini iliingia katika huzuni baada ya mfalme wao kuwa katika harakati za mwisho za maisha yake. Mfalm huyu aitwaye Zulain mwenye miaka yapata elfu tatu alikuwa katika ugonjwa kwa muda wa miaka kumi  sasa leo ndiyo dalili za kufikia mwisho wa uhai wake zilionekana dhahiri kwa majini wote wa hapo kwenye kasri hilo. Akiwa kalala kwenye kitanda chake cha thamani kwa muda wa miaka kumi kutokana na ugonjwa uliokuwa unamsumbua ambao haujulikani, kwa mara ya kwanza aliinuka kitandani ghafla akakaa kitako kisha akasimama akaelekea kwenye kiti chake cha enzi akiwaacha watumishi wake wakiwa na simanzi sana. Kuugua mfalme kwa muda mrefu kisha kuinuka ghafla ni dalili tosha ya kuwa siku za mwisho za miaka yake zimekaribia, hivyo hata watumishi wa ndani ya kasri hili walitambua kuwa siku za mwisho za uhai wa mfalme wao zimekaribia.

Hata mfalme mwenyewe alitambua kuwa ana masaa ya kuishi duniani au siku ya kuishi duniani hivyo alitaka kuongea maneno ya mwisho kabla roho yake haijaachana na mwili wake, alipokaa kwenye kiti chake jambo la kwanza kulitamka ilikuwa ni kuitiwa mawaziri wake wote pamoja na viongozi wengine waliopo chini ya utawala wake ili awaambie jambo la muhimu pamoja na kuacha kauli ya mwisho katika himaya yake. Amri ya kuitwa mawaziri na viongozi wa juu katika himaya yake ilitekelezwa mara moja na baragumu maalum likapulizwa kwa haraka sana na mpulizaji  wake anayetoka katika himaya hiyo, ndani ya sekunde kadhaa chumba cha mkutano kilijaa mawaziri na viongozi wenye nyadhifa kubwa katika himaya hii ya kijini ambao walikuwa ni majini wa aina mbalimbali.
"Himaya ya Majichungu inaelekea kukumbwa na simanzi kubwa kwani kiongozi wake niliyetawala kwa muda wa miaka 2500 nakaribia kufa na dalili kuu ya kufa kwangu nadhani imeonekana kabisa dhahiri kwenu na kwa watumishi wangu, sasa basi suala la kutafutwa mrithi wa taji langu na  kiti changu cha enzi nawapa nyinyi. Nahitaji mjukuu wangu Zalabain ambaye ndiye mrithi wa kiti changu cha enzi na taji langu apatikane haraka iwezekanavyo kwa namna yoyote na afutwe popote alipo aletwe huku akabidhiwe jukumu lake la ufalme kwani mwanangu Zaif ambaye ndiye baba mzazi wa Zalabain hatunaye  na wote mnatambua ni jinsi alivyougua hadi akata roho katika himaya hii. Sasa basi Zaif kabla hajafa alisema duniani yupo mjukuu wangu aitwae Zalabain, sasa inabidi huyo mjukuu wangu atafutwe.kwa hali yoyote hadi apatikane ili aje kuchukua wadhifa wangu kama mrithi pekee aliyebakia. Pia nahitaji  mila na desturi za himaya hii zibaki kama nilivyozikuta na zisibadilishwe kwa namna yoyote na wala asitokee kiumbe akabadilisha au akamshawishi kiumbe yoyote abadilishe. Mwisho kabisa nahitaji Sadik bin Zultash baba wa mapacha Saliim na Salmin aachiwe huru kuanzia sasa kwani uzao wake kwa faida moja umetusaidia kwa kutuletea jini mwenye nguvu kuliko wote na anayeifanya himaya yetu isidhuriwe na  kiumbe wa aina yoyote, sina la ziada ni hayo tu" Mfalme Zulain alihitimisha na kikao kikamalizika mara moja karibia viongozi wote wakatawanyika wakiwa na simanzi juu ya mfalme wao. Siku iliyofuata ilikuwa ya simanzi zaidi  kwa himaya nzima ya Majichungu kutokana na kifo kilichomkumba mfalme wao, himaya nzima iliomboleza kifo hicho kwa muda wa wiki saba na baada ya hapo jeshi la majini watatu ambao ni makomandoo likaundwa kwenda kumtafuta Zalabain popote alipo ili aje kurithishwa ufalme wa babu yake.

****


WIKI MOJA BAADAYE
  USIKU WA MANANE
     AMBONI
      TANGA
  Eneo la miamba yenye mapango ya kihistoria jijini Tanga  jirani kabisa na mto mkubwa Tanga nzima uitwao mto Sigi kulikuwa kuna kundi la vijana kumi waliokuwa wameuzunguka mti mmoja wa mkoko ambao unasadikika kuwa mti wa ajabu kutokana na kuota eneo ambalo lipo mbali na ufukwe wa bahari. Vijana hao walikuwa wameuzunguka mkoko huo ambao ulikuwa umening'inizwa chupa ya ukubwa wa lita moja ambayo ilikuwa ikijibadili rangi kila kukicha, walikuwa wamejifunga kaniki nyeusi kiunoni na vitambaa  vyekundu kichwani na kwenye mikono yao. Muda wote walikuwa wapo makini kuitazama chupa hiyo pamoja na mazingira ysnayozunguka mto  Sigi  pamoja na upande wa mapango ya Amboni, walikuwa wapo kimya sana na umakini wao katika kuangalia mazingira ya hapo ndiyo ulizidi kwani walikuwa wanapambana na wachawi wa kila namna ili kuilinda chupa iliyopo hapo mtini ambayo huonekana usiku kwa wenye uwezo kuiona na mchana haikuonekana kabisa.
Siku hiyo majira ya saa nane usiku vijana hao walimshuhudia Mamba  mmoja mkubwa akitoka ndani ya mto Sigi na akakaka pembezoni mwa mto huo mita chache kutoka  pale walipo, wote walimpuuzia mamba huyo kutokana na dawa zao wanazotumia hawezi kuwaona. Walibaki wakimtazama yule Mamba kwa  jinsi alivyo mkubwa huku kuliko hata Mamba wote waliowahi kuwashudia katika mto Sigi tangu wakiwa watoto, mmoja kati ya wale vijana alishikwa na shauku ya kwenda kumtazama  yule Mamba na akasogea karibu zaidi kwani dawa zao zilikuwa zinawazuia wasionwe na wanyama wakali. Alisogea akamtazama zaidi na akabaini ni mamba wa ajabu mwenye rangi tofauti na Mamba wa pale mtoni, akiwa anashangaa uajabu wa yule mamba ghafla alijikuta akipigwa mkia akatumbukia mtoni na mamba huyo naye akazama mtoni akiwaacha wale vijana waliobakia wakikimbia hadi pembezoni mwa mto wakiacha kuilinda ile chupa. Hilo lilikuwa kosa jingine kwao na hawakupata hata nafasi ya kulirekebisha kwa balaa lililotokea, kimbunga kikali kilivuma kuuzunguka ule kwa muda wa dakika kadhaa na kilipoacha ile chupa wanayoilinda ilikuwa imepasuliwa tayari. Kabla hata hawajatafakari kitu cha kufanya maji ya mto Sigi nayo yalianza kuzunguka kisha yakanyanyuka juu urefu wa mlima huku yakizunguka na yakatengeneza umbo la jitu kubwa ambalo mkono mmoja lilikuwa limemshikilia kijana yule aliyepigwa mkia na Mamba akaingia mtoni. Vijana walipoona hivyo wakajua wameingiliwa na kazi yao imeshaharibika hivyo walitaka kukimbia ili kujiepusha na hatari kwani viumbe waliowavamia sio wa kawaida, walikimbilia upande lilipo pango wakijua ni salama kwao ili wapate sehemu ya kutorokea. Walipokaribia kuingia pangoni walikutana uso kwa uso na nyoka mwenye vichwa kumi na ikawabidi wakimbilie mtoni kwa upande mwingine bila ya kutambua wanajipeleka kwenye eneo la kifo, vijana hao walijitupa mtoni kwenye maji wakiwa wanataka kuokoa maisha yao tu na wala hakukumbuka kuwa dawa waliyojipaka ya kuzuia wasidhuriwe na wanyama wakali inatoka mwilini ikiwa utaingia kwenye maji. Walipokuja kukumbuka tayari walikuwa wamezungukwa na mamba zaidi ya kumi wa mto huo, walikuwa wamejirusha sehemu yenye maskani ya Mamba bila ya kujijua na wakawa kitoweo cha Mamba.

****

Sherehe kubwa ilifanyika katika kasri la kifalme la Majichungu katika kusherekea kupatikana kwa mjukuu anayepaswa kurithi kiti na taji la ufalme wa babu yake, ilikuwa ni mara ya  kwanza kwa mjukuu huyo mwenye mchanganyiko wa binadamu na jini kufika katika himaya tangu azaliwe. Sherehe ilipoisha ndipo taratibu zote za kimila na desturi za kumpatia ufalme Zalabain zikaandaliwa kama ilivyofanyika kwa wafalme waliopita. Siku iliyofuata sherehe nyingine ya kuvikwa taji la ufalme ilifanyika katika uwanja mkubwa uliopo nje ya kasri la kifalme ambayo ilihudhuriwa na wanahimaya hiyo karibia  wote, kiti cha kifalme kilitolewa kikawekwa sehemu yenye jukwaa lililopambwa kwa busati lenye rangi nyeupe. Muda wa kuvikwa taji Zalabain ulipowadia Mkuu wa baraza la sheria la himaya  hiyo aliingia akiwa amebeba taji la kifalme liliwekwa kwenye kasha lililopambwa na fito zenye rangi nyekundu, Zalabain akiwa nyuma ya Mkuu huyo wa baraza la sheria pembeni yake akiwa na walinzi wenye miili mikubwa pamoja na sura za ajabu. Zalabain na mkuu huyo walipanda katika jukwaa lenye kiti cha kifalme huku mamia ya wanahimaya ya Majichungu wakishangilia kwa nguvu, aliamriwa aketi kwenye kiti cha ufalme naye akatii akaketi na Mkuu wa  baraza la sheria akashika kasha lenye  taji la kifalme akasogea kisha akawageukia Wanahimaya ambao wapo hapo kushuhudia tukio hilo.
"Leo ni siku maalum na ya kihistoria ya kumpata kiongozi wetu aitwae Zalabain bin Zaif atakayeiongoza himaya yetu akirithi utawala wa Babu yake Zulaif, akiwa na miaka 26 tu atakuwa kiongozi mdogo kuwahi kutokea katika Himaya yetu hii  hivyo naomba mumpokee" Mkuu wa baraza la sheria aliongea kisha akamgeukia Zalabain ambaye tayari ameshavaa mavazi ya kifalme  akawa anatazama nae.
"Kwa mamlaka niliyokabidhiwa ninakukabidhi  na kukuvisha taji hili la Kifalme litakalokufanya uwe mfalme, miongoni mwa wafalme, wa ukoo wa kifalme, waliowahi kuwa wafalme, uwe kiongozi wa kasri la kifalme. Zalabain sasa wewe ni mfalme wa himaya ya Majichungu" Mkuu wa baraza la sheria alipomaliza kusema maneno hayo aliliweka taji kichwani mwa Zalabain huku halaiki ya wanahimaya wakishangilia, kushangalia huko kulizimika ghafla mithili ya umeme unavyozimika eneo lenye giza. Wote walibaki wameduwaa baada ya taji la kifalme lililowekwa kichwani mwa  Zalabain kuruka kando likaanguka kwenye busati lililotandazwa hapo jukwaani. Mkuu wa baraza la sheria aliona ni jambo la kawaida sana na aliinama akalishika ili alinyanyue lakini taji halikuinuka na lilikuwa zito sana na ikambidi alishike kwa mikono miwili na akashindwa kuliinua vilevile. Aliamua awaite wale walinzi walioingia na Zalabain walinyanyue nao wakashindwa pia kulinyanyua eneo hilo. Wanajeshi wanaoaminika wana nguvu sana nao walishindwa kulinyanyua taji hilo, Zalabain mwenyewe alibaki akiwa anashangaa kwa tukio hilo ambalo hakulielewa limetokana na nini.
Mnajimu mkuu wa Himaya hiyo aliitwa mara moja na akapewa kazi ya kulitatua tatizo hilo kwani yeye ndiye anayeaminika katika himaya hiyo, mnajimu huyo wa kijini alianza kulizunguka taji hilo la kifalme kisha akajaribu kuliinua lakini alishindwa kabisa na akaanza kubadilisha macho yake yakawa kama ya paka akamtazama Zalabain.
"Siyo uzawa wa ukoo wa mfalme huyu ndiyo maana taji limemkataa na wala siye mtoto halisi wa Zaif, taji hili linahitaji abadilishwe kiongozi kwani kizazi cha ukoo wa mfalme alibaki Mfalme Zulain tu ambaye amefariki tayari. Ufalme unatakiwa uhamishwe katika koo nyingi.." Mnajimu alishindwa kumalizia kauli yake na akajikuta amepigwa kofi zito hadi akaanguka chini,  akiwa hajajua nani aliyempiga akahisi anakabwa shingoni huku akinyanyuliwa juu. Walinzi walipoona hali hiyo walitaka kusogea ili wamdhibiti kiumbe anayemkaba Mnajimu mkuu lakini walisita baadaya kiumbe mwenyewe kujitokeza hadharini, Salmin ambaye anajulikana na wanajamii hiyo kama jini mwenye nguvu kuliko wote ndiye aliyeonekana akimkaba Mnajimu huyo shingo.
"Kwanini unasema uongo ilihali wewe ni Mnajimu unayeheshimiwa na kuaminiwa katika himaya hii" Salmin alimuuliza Mnajimu huku akizidi kumkaba, Mnajimu aliomba aachiwe ili aongee na alipoachiwa ndipo akamwaga uhalisia wa jambo lenyewe.
"Wanahimaya na wakuu wote naomba mnisamehe sana kwa  kusema uongo juu ya mjukuu wa mfalme, tamaa ya madaraka ndiyo imesababisha niseme uongo. Niliahidiwa kupewa nafasi ya mkuu wa baraza la sheria ikiwa tu nitafanya hila ufalme uhamishiwe katika ukoo wa waziri mkuu ili waziri mkuu awe mfalme wa Himaya hii, narudia tena viongozi wangu na wanahimaya wenzangu naomba mnisamehe kwani mimi nina nafsi na tamaa ni kitu cha  kawaida kwa mwenye nafsi" Mnajimu alitoa maelezo hayo akiwa na aibu usoni  kutokana na jambo alilolifanya, kuomba kwake msamaha hakukusaidia kitu kwani alikamatwa yeye na Waziri mkuu  baada ya mkuu wa baraza la sheria kutoa amri hiyo. Baada ya kukamatwa kwa Waziri mkuu na Mnajimu mkuu Salmin alilitazama taji la kifalme kisha akamtazama Zalabain kwa umakini, macho yake yalianza kutoa nuru mithili ya almasi iliyomulikwa na mwanga mkali.
"Zalabain.......Zalabain mrithi wa kiti cha mfalme aliyestahiki kuvishwa taji la ufalme wa himaya hii lakini taji limemkataa kutokana na jambo moja tu ambalo mrithi wa kiti hiki hatakiwi kuwa nalo kabisa ambalo wewe unalo, udhaifu.....udhaifu wako ndiyo chanzo cha taji hili kukukataa. Ikiwa unatakiwa kuwa mrithi wa taji hil na kuna ubaya ambao umetendewa unatakiwa ulipe kisasi kwanza na si kusamehe ili upate taji hili, baba yako Zaif  ameangamizwa na wanadamu akiwa na miaka 1500 na wanadamu hao ndiyo chanzo cha taji hili kukukataa na pia kuwa zito kuinuka kwa yoyote mwenye wazo la kuliweka kichwani mwako. Kisasi cha ubaya uliofanyiwa ndiyo kinahitajika ili hili taji likae kichwani mwako na hakuna mwingine atakayelivaa isipokuwa wewe, unapaswa utambue kwamba himaya hii yote inahitaji kiongozi na haiwezi kuendelea bila kiongozi na pia kiongozi ni wewe unatakiwa ulipe kisasi ili watu wako uwaongoze na si usamehe wapotee. Je upo tayari kuongoza himaya hii?" Salmin alifafanua chanzo cha  kutokea jambo lililotokea kisha akamuuliza Zalabain.
"Nipo tayari kuongoza, nipo tayari kisasi cha kuuawa kwa baba yangu na nipo tayari kulipa kisasi cha ubaya uliotendwa kwangu" Zalabain aliongea huku macho yakibadilika na kuwa mekundu kabisa na yenye kung'aa, Salmin alimsogelea akamshika mkono kwa sekunde kadhaa kisha akamuachia halafu akamuambua "kazi njema".  Salmin aliliokota taji la kifalme akamkabidhi Mkuu wa baraza la sheria kisha akaondoka, sherehe hizo ilivunjwa hapohapo na Zalabain akahitajika atimize kile alichoahidi mbele ya majini wote wa himaya hiyo.


****


  Asubuhi ya siku iliyofuata tangu litokee tukio la kutoveshwa Zalabain taji, wafanyakazi wa kampuni ya upangishaji nyumba iitwayo Extoplus walikuwa wanasafiri kuelekea katika kijiji cha Duga Maforoni kwenda kuhudhuria sherehe ya uzinduzi wa nyumba mpya za kupangishwa  za ksmpuni hiyo. Siku hiyo wafanyakazi wote waliotakiwa kwenda kwenye sherehe hiyo walijawa na hofu, karibu kila mfanyakazi alikuwa anasita kwenda anasita kwenda kwenye sherehe lakini hawakuwa na uwezo wa kukataa kwani ni idara nzima imeteuliwa kuhudhuria sherehe hiyo. Saa mbili kamili wote walikuwa kwenye basi wakielekea Duga kuhudhuria sherehe hizo, ndani ya basi kimya kilitawala kuanzia mwanzo wa safari  na kilikuja kuvunjwa baada ya gari aina ya toyota coaster waliyokuwa wanaitumua kuvuka daraja la Utomfu. Mwanamke mmoja wa makamo alivunja ukimya uliopo ndani ya gari kwa kusema, " jamani mimi jana usiku nimeota ndoto ya ajabu sana".
"mmh! Hebu tueleze ni ndoto gani hiyo" Mwenzake aliyekuwa pembeni naye alidakia.
"nimeota nashuka kwenye gari natoka kazini nikakutana na mtoto wa  miaka sita hizi akaniamkia kwa uchangamfu na mimi nikaitikia, yule mtoto kaniuliza unaujua mtego wa panya mimi nikamjibu ndiyo. Akaniuliza je kiumbe chochote kikiugusa unamnasa au unanasa panya tu, nikamjibu yoyote akiugusa ananaswa haijalishi kama Panya au siyo panya. Nilipomjibu akatabasamu nikamuuliza mbona umeniambia hivyo, akanijibu safari yako  ya kesho Duga ni mtego wa panya ukienda utanasa ingawa wewe sio panya. Nimeshtuka usingizini hapohapo nikawa najiuliza kuhusu ndoto hiyo jamani ina maana gani" Yule mwanamke alieleza ndoto yake na alipomaliza wafanyakazi wote walikuwa wameingiwa na woga hapohapo.
"jamani hata mimi hii ndoto nimeiota" Mwanamke mwingine akadakia huku akionesha kuogopa.
"hata mimi" Mwanaume wa makamo ambaye ni mmoja wa wafanyakazi hao naye akadakia na mwishowe wote kwa pamoja wakatamka kwamba wameiota ndoto hiyo na hofu ikawa imetawala nafasi zao huku wengine wakimsihi dereva ageuze gari wasiende. Walikuwa wameshafika Amboni na sasa wapo kwenye daraja la kulia la mto Sigi hivyo dereva alikuwa yupo makini kulimaliza daraja hilo na hakuwasikiliza kabisa, baada ya kulipita daraja ndipo dereva akasema "jamani hata mimi nimeota ndoto ya namna hiyo lakini nimeipuuzia kwani si kila ndoto ni ya kweli".
"unasemaje wewe hebu simamisha nishuke nipande mabasi yanayotoka Horohoro nirudi mjini" Mwanamke yule aliyeeleza kuhusu ndoto alikuja juu.
"sawa ngoja tufike Mpirani kwenye kituo ili upate hilo gari" Dereva akimwambia yule mwanamke lakini hakutaka kumuelewa.
"simamishe gari nakuambia!" Yule mwanamke alizidi kufoka, dereva hakuwa na jinsi ilimbidi akanyage breki lakini gari ilikataa na ndiyo mwendo ulikuwa unazidi na usukani ikawa unajiongoza wenyewe.
"we mwanaharamu wewe simamisha gari nishuke sio kuongeza mwendo" Yule mwanamke alizidi kufoka baada ya kuona mwendo wa gari unazidi kuwa mkali, dereva hakumjibu yule yeye alitoka kwenye usukani akasimama kisha akawaangalia wafanyakazi wa idara nzima akiwa na hofu.
"si mimi ninayeendesha jamani gari linaenda lenyewe hili hebu oneni" Dereva aliongea huku akiwaonesha wafanyakazi wote jinsi usukani ulivyokuwa unajiongoza wenyewe, wafanyakazi wote walipoona hicho kioja walijikuta wakijaribu kutoka nje lakini walishindwa kwani milango haikufunguka na vioo vyote vilijifunga ghafla hata vile vilivyokuwa wazi vyote vilijifunga. Wafanyakazi wote walijaribu kupiga vioo ili wavunje lakini walishindwa kwani vioo vilikuwa vigumu sana, gari nayo ilizidi kuongezeka mwendo hadi ikawa kama ipo kwenye mashindano.

*Mwanzo tu ni balaa je huko mbele


ITAENDELEA !!


No comments:

Post a Comment