Sunday, December 4, 2016

WAKALA WA GIZA SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA





RIWAYA: WAKALA WA GIZA

MTUNZI: HASSAN O MAMBOSASA


SIMU: +255713776843
          +255762219759


WHATSAPP: +255713776843

SHUKRANI ZOTE ANASTAHIKI MWENYEZIMUNGU MUUMBA WA ULIMWENGU WOTE KWA KUNIWEZESHA KUANDIKA RIWAYA HII NIKIWA NA AFYA NJEMA




______________+18__________________



SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA!!

            "Usiwe na hofu Farida tutakutana siku nyingine ngoja nikupe ya matumizi, asubuhi wewe nenda chuo tu ukaendelea na masomo" Wilson aliongea huku akivaa nguo zake, alipomaliza aliingiza mkono mfukoni akatoa kitita cha pesa ambacho alimpatia Farida kisha akambusu mdomoni binti
huyo ambaye angeweza hata kuwa mpwa wake. Wilson hakutaka kupoteza .muda alichukua funguo zake za gari akatoka chumbani humo usiku huohuo, alitembea kwa haraka hadi yalipo maegesho ya magari akaingia ndani ya gari yake akaiwasha akaiondoa eneo hilo

_____________
 ______________
_____________
    ________

    Safari ya Wilson iliishia  yalipo makao ya muda ya vijana wa kazi waliopeww, akionekana ni mwenye kuchanganyikiwa Wilson alipiga honi mfululizo alipofika kwenye lango la nyumba ambayo ndiyo kambi ya vijana wa kazi walioletwa nchini. Lango la kambi hiyo ambayo imebeba nyumba ya kifahari ndani yake lilifunguliwa kwa haraka baada ya kutambuliwa ujio wake  na mlinzi wa eneo hilo, Wilson aliingiza gari ndani kwa kasi ya ajabu hadi mbele ya kibaraza cha nyumba hiyo ambapo alilisimamisha kwa ghafla, alishuka ndani ya gari hiyo akawakuta Benson na wenzake tayari wakiwa wanamsubiria eneo hilo.

           "Nyinyi yuko wapi Benjamin na Leopard Queen?!" Wilson aliuliza kwa jazba huku akihema kwa nguvu.

          "Wilson usiwe na papara namna hiyo tuambue kuna nini?" Santos aliuliza.

            "Nimewauliza na nyinyi mnaniuliza swali tena, Benjamin na Leopard wako wapi?!" Wilson aliuliza tena akiwa na jazba sana, muda huo huo mlango wa kuingia ndani ulifunguliwa na Filbert Ole akatoka ndani akajongea hadi eneo walilopo  Wilson na kina Santos.

            "Wilson kuna nini tena mbona wahka mwingi mdogo wangu?" Filbert Ole aliuliza.

             "Kakaa nimepigiwa kwa namba ya Leopard Queen nimepokea nikijua ni yeye kumbe ni N001" Wilson aliongea kwa kulalamika, watu wote waliposikia namba hiyo ya N001 walishtuka kisha wakamtazama Wilson kwa umakini sana.

              "Eeeh! Ni..niambie kakuambiaje" Benson aliuliza akiwa na kigugumizi baada ya kubaini mtu hatari alitumia simu ya mpenzi wa pacha wake, Wilson alipokuwa akijiandaa kuendelea kuongea yeye alimuona kama anachelewa kuongea. Kumuharakisha kuongea ilimbidi amshike mkono kwa nguvu na akimtikisa huku akiita jina lake, Wilsom aliona ilikuwa ni kero akautoa mkono wa Benson ulipokuwa umemkamata na akaweka mambo wazi.

              "Ameniambia nikafuate masalia nyumbani kwa Leopard Queen" Wilson aliongea huku akikaa kibarazani bila kupenda kutokana kuchanganywa na habari hiyo, waliobaki wote waligwaya kutokana na taarifa ile hasa Benson ambaye alichanganyikiwa kabisa baada ya kusikia hivyo. Ama kweli damu ni nzito kuliko maji, kijana mwenye mgumu uliokomazwa na mafunzo mbalimbali pamoja na kazi za hatari alipatwa na uchungu alipisikia taarifa hiyo inayohusu eneo ambalo pacha wake na Leopard Queen wapo.

     Benson aliweka mikono kichwani baada ya kusikia taarifa hiyo huku moyo wake ukiwa hauamini kabisa kwani alitambua mtu aliyetembelea nyumba hiyo ni mtu hatari sana, macho yake yalianza kuwa mekundu taratibu uchungu wa kusikia habari hiyo ulimkolea.  Aliwatazama wenzake ambao nao walikuwa wamepigwa butwaa ya ghafla na taarifa hiyo na hawakuwa wakizungumza chochote, kimya chao kilimfanya atoe bastola yake  aina ya Desert Eagle akaifungua magazine akaitazama risasi. Aliporidhika risasi zipo aliirudisha magazine ndani kisha akaikoki akaimuelekezea Wilson alipokuwa amekaa kibarazani huku akihema kwa nguvu, wote walipigwa na butwaa kwa kitendo hicho cha Benson na walipotaka kumsogelea alinyanyua bastola akawaelekezea wote.

              "Sitaki kumwaga ubongo wa mtu jamani nyote wekeni mikono kichwani wakati nadili na Wilson" Benson aliongea kwa hasira.

             "Benson" Filbert Ole aliita.

               "Kimyaa! Hamujui kwamba kaka yangu yupo kwenye hatari? Hamujui kama N001 ni mpelelezi hatari mwenye ujuzi wa kila mwanausalama, mnafikri pacha wangu atakuwa salama mbele ya mtu huyo" Benson aliongea kwa hasira kisha akaelekeza bomba la bastola alipo Wilson.

              " Wilson nipe funguo za gari lako upesi" Benson alitoa amri papo hapo, Wilson alianza kutetemeka na mwishowe alitoa funguo akamkabidhi Benson ambaye aliichukua kwa nguvu kama kibaka anakwapua simu mkononi.

    Benson alijongea kwa haraka hadi lilipo gari la Wilson kisha akabonyeza  rimoti ya kufungua milango huku akiwaangalia wenzake waliobaki akimshangaa, alipogusa kitasa cha mlango kufungua aingie ndani ya gari Santos alipiga hatua  moja mbele. Hatua hiyo iligundulika na Benson ambaye aligeuka nyuma kwa haraka akalifyatua risasi chini ikatua kwenye  sakafu maalum iliyopo mbele ya kibaraza, sauti kubwa ya mlipuko wa bastola ilisikika ambayo ilimfanya Santos agande hivyo hivyo asiendelee na hatua ya pili. Wengine wote waliobaki walipatwa na mshtuko kutokana na mlipuko huo wa bastola, Wilson kwa uoga alirudi zaidi nyuma kwa kusota na makalio akipanda ngazi mbili za kibaraza akiwa na uoga mkubwa.

              "Nimesema asinisogelee mtu" Aliongea kwa ukali kisha akaingia ndani ya gari akafunga milango yote pamoja na vioo akiwaacha wenzake wakiwa wamepata ujanja wa kuweza kusogea mbele lakini hawakuweza kuingia ndani ya gari hiyo. Benson aliwasha gari kisha akalirudisha nyum kwa kasi akaigeuza katika eneo hilo la maegesho, geti tayari lilikuwa limeshafunguliwa hadi muda huo na ikawa rahisi kwake kutoka ndani ya nyumba hiyo kwa kasi sana akiwaacha wenzake wakimshangaa hadi alipopotea katika upeo wa macho yao.

             "Wote muende nyumbani kwa Leopard Queen upesi sana" Filbert Ole alitoa amri, vijana wa kazi pamoja na Wilson waliondoka hadi kwenye banda maalum la magari wakafungua milango. Wote kwa pamoja waliingia ndani ya mandhari yenye magari mbalimbali yaliyoegeshwa na walichangua gari ambayo waliingia wakawasha kisha wakaliondoa eneo hilo kuelekea getini ambapo walitoka wakafuata uelekeo wa barabara aliyopita  Benson.


****

    Baada ya kuacha balaa na kutoweka mara moja akimpigia simu mmoja wa mbaya wake, Norbert aliamua kuelekea moja kwa moja Kurasini katika nyumba ya kampuni. Ndani ya dakika kadhaa tayari alikuwa ameshaingia katika nyumba hiyo akaegesha gari katika maegesho, alishuka kwenye gari moja kwa moja akazama ndani ya nyumba hiyo kwa lengo la kukutana na mwenzake.

    Muda anaoingia ndani ya nyumba hiyo ndiyo muda ambao Benson alipatwa na kiwewe baada ya kusikia ujio wa N001 ambayo imesimama mbadala ya utambuzi wa Norbert kikazi zaidi, alipoingia ndani ya nyumba hiyo alikutana na  Moses pamoja na M.J Belinda wakiwa wamekaa sebuleni katika makochi tofauti wakijadili mambo. Norbert alijongea mita chache kutoka pale walipo kisha akasimama akaweka mikono kiunoni akiwatazama kila mmoja halafu akawanyooshea vidole, alitoa tabasamu kisha akatikisa kichwa kusikita akiwatazama.

             "Ndiyo nini hivyo?" M.J Belinda aliuliza.

             "Aisee mna balaa" Norbert aliongea huku akisikitika.

                "Sikusomi ujue" Moses naye alimuambia Norbert akitumia lugha ya misimu akimaamisha hamuelewi.

                "Hivi toka lini Simba akakaa na Pundamilia aliyenona hata asimpige kucha maana anamtamanisha  hata akiwa ameshiba" Norbert aliongea kimafumbo akiwalenga Moses na MJ Belinda ambao walikuwa wamekaa pamoja, wote  waliposikia maneno hayo walibaki vinywa wazi na M.J Belinda ndiyo akamfuata kwa kasi.

               "Muhuni mkubwa ndiyo yaliyopo kichwani mwako hayo kila siku" M.J Belinda aliongea huku akimkaribia  ambaye alikuwa anacheka alipoongea hayo maneno, alipomfikia alirusha kibao cha kilegevu ambacho Norbert alikikwepa kisha akaanza kukimbia kuzunguka sebuleni hapa. M.J Belinda alimkimbiza. Norbert alikimbia kuzunguka  sebule hiyo hadi pale M.J Belinda alipoacha kumkimbiza ndipo naye alisimama, wote walirudi kwenye kochi wakaketi kisha macho yakawa yanaelekea kwa Norbert.

              "Ujio wako una jambo si bure" Moses alimwambia Norbert.

              "Nimekuja kuwaambia kazi imeanza" Norbert aliongea.

              "Aaah! Wewe kuna la ziada nafikiri unahitajika kutueleza" Moses aliongea

                 "Yeah ndiyo lipo na ni hili hapa, Benson ana pacha wake anaitwa Benjamin ambaye tayari kwa sasa si miongoni mwa viumbe hai hivyo mchakamchaka umeanza kuna ulipaji kisasi" Norbert aliongea.

               "Umemkata fyuzi tayari siyo?" Moses aliuliza.

                "Of Course ningechelewa angenikata yeye kwani alikuwa na mguu wa kuku" Norbert aliongea.

                 "Na sisi tuna jipya nafikiri linahitaji msaada wako kwani wewe ndiyo mtaalamu wake pekee" Moses aliongea.

               "ni lipi au kuna chuma hakitaki kunyooka" Norbert aliongea.

                 "Kama ulikuwepo hebu twende basement ukakione nafikiri kwa mtaalamu wake kitanyooka" Moses aliongea huku akisimama, Norbert na M.J Belinda nao wakasimama.

    Wote kwa pamoja waliifuata korido ndefu iliyoanza hapo sebuleni  hadi  mwisho, walikuta ngazi ambazo walizishusha hadi chini kiasi cha ghorofa moja. Walikuta mlango ambao waliufungua wakatokea kwenye korido nyingine fupi iliyotenganisha vyumba kadhaa, waliifuata korido hadi mlango wa pili upande  wa kulia uliotengenezwa kwa chuma. Moses aliufungua mlango hyo mzito kwa namba maalum kisha akaingia ndani wenzake wakifuatia, waliingia katika chumba chenye giza ambacho kilipowashwa taa alionekana yule mzungu aliyebaki mzima baada ya kuachiwa kichapo na Moses akiwa amefungwa kwenye kiti cha chuma kilichopo pembeni ya mapazia yanayotumika kwenye wodi za hospitali. Tayari alikuwa ana fahamu zake ingawa alikuwa ana majeraha mbalimbali kutokana na mateso aliyopewa, Norbert alipomuona mzungu huyo alimtazama huku anatabasamu tu.

              "Chuma chenyewe kisichonyooka ni hichi au kingine?" Norbert aliuliza kwa dharau sana huku akimnyooshea kidole mzungu yule.

            "hiko hiko" M.J Belinda alimjibu.

              "nilidhani ni chuma cha pua kumbe ni hichi cha kawaida" Norbert  aliongea kisha akavaa koti la kitabibu lililopo ukutani mwa chumba hicho, alitembea hadi kwenye kona moja ya chumba hicho yenye meza iliyofunikwa na kitambaa ambayo aliisukuma hadi mitaa kadhaa kutoka yule mzungu alipo.

      Mzungu huyo ndiye yule aliyepigwa goti la uso  na M.J Belinda kabla wenzake wawili  hawajauawa na Mose, alikuwa ameleta kiburi cha kutotaka kuongea neno lolote baada  ya kubanwa na Moses kwa kushirikian ns M.J Belinda ambao hawakuwa na utaalamu sana katika masuala ya kubana watuhumiwa hadi pale alipofika Norbert mtaalam aliyesomea masuala  hayo kiziada  nchini Cuba wakati akisomea ukomandoo ngazi ya juu kabla hajapelekwa Japan kujifunza Ninjutsu(Uninja).

     Tangu ahitimu mafunzo hayo hakuna mhalifu aliyewahi kubanwa na yeye akakataa kusema ukweli, wahalifu tofauti ikiwemo Tasi katika kisa cha JINAMIZI na mzungu Scott katika kisa cha SHUJAA walikuwa wabishi lakini waliongea wenyewe walipopewa kibamo kikali sana. Sasa akiwa na meza ya mteso pamoja na nguo maalum za kutesa watu tayari yupo mbele ya Mzungu aliyeleta ubishi, Norbert alimtazama tena yule mtu kisha akatabasamu zaidi halafu akachukua kibanio kimoja maalum kwa kutolea meno akawa anajongea kumsogelea yule mzungu.

              "Hana jino hata moja huyo" Moses alimuambia Norbert ambaye alisita akarudi kwenye meza ile yenye vifaa akakirudisha kifaa alichokichukua.

               "Kwahiyo kawa kibogoyo na bado anagoma, dawa mbili nampa ataongea mwenyewe" Norbert aliongea kisha akaenda ukutani akawasha swichi ya umeme, Yule mzungu alipigwa shoti sana lakini hakunyanyua mdomo wake kusema.

        Wakati shoti za umeme ambazo zilikuwa zimeunganishwa na kiti cha umeme zikiendelea kumsulubu vilivyo yeye alipiga kelele sana, alipoachiwa alikakaa kimya na hakusema chochote kuonesha yeye ni jeuri sana. Hali hiyo ilimfanya   Norbert amtese pasipo huruma hadi alipoishiwa nguvu ndiyo akamuachia, alibaki  akiwa anamtazama tu yule Mzungu kisha akasikitika.

              "Tumekwambia hicho ni chuma imara" Moses alimuambia Norbert.

                 "Kila kitu kina namna yake huyu atasema tu" Norbert aliongea kisha akavua mipira aliyovaa mikononi, alitoka ndani ya chumba hicho  kwa dakika kadhaa na aliporejea alikuwa amebeba mtungi wa gesi pamoja na jiko lake.

     Aliwaacha Moses na M.J Belinda vinywa wazi lakini yeye hakuwatilia maanani, alifika hadi mbele ya Yule mzungu kwa mitaa kadha akaunganisha mpira wa gesi wa jiko na mtungi halafu akalijaribisha kuliwasha.

              "We Nor unataka kufanya nini?" M.J Belinda aliuliza

               "Bibie kuwa mtazamaji ingawa hii hutaona kila kitu" Norbert alimuambia M.J Belinda kisha akaliweka jiko la gesi chini ya kiti cha chuma ambacho kina madini ya bati katika sehemu ya kukalia. Wenzake walikuwa wanamshangaa lakini hakujali hata kidogo yeye aliendelea na kazi yake, alifunika mashuka ya hospitali yaliyokuwepo humo ndani ili waliopo nje wasione kinachoendelea.

              "Nor unajua sikuelewi" M.J Belinda aliongea.

                "Aaah! Bibie kuwa na subira hichi chuma nimekiletea asidi ili kiyeyuke kabisa" Norbert aliongea, kuteswa kwa namna hiyo ambapo Moses hakuwahi kupaona kulimvuta aingie ndani ya mapazia kuja kutazama.

      Hakika ilikuwa ni mbinu ambayo hajawahi kuiona ikitumika kwenye mateso, alisimama ndani ya kingo moja ya mapazia hayo akiwa na shauku kubwa ya kutazama jinsi ambavyo mbinu hiyo ilivuokuwa ikifanya kazi.

     Norbert aliliwasha lile jiko la gesi ambalo liliwaka lakini moto wake haukugusa sehemu ya kukalia ya kiti hicho cha mateso, alimvua yule mzungu suruali aliyovaa hadi  magotini kilazima akabaki hana nguo na makalio yake yakawa yamegusa sehemu ya bati ambayo hutumika kukalia katika kiti hicho chuma.

           "Eleza kila unachokijua kwenye mpango wenu" Norbert alimwambia akiwa ameshikilia chuma kimoja kifupi kilichosimama pembezoni mwa kiti hicho, Mzungu yule bado alileta jeuri kisha akatema ambayo Norbert aliyakwepa. Kitendo hicho kilimfanya Norbert atabasamu kisha  akachuchuma akaongeza moto kwenye jiko la gesi, akiwa na tabasamu lake lilelile usoni mwake alikishika kile chuma kifupi cha pembezoni mwa kiti akakipeleka kulia mara moja. Kiti cha mateso kilianza kushuka chini taratibu kikaufikia ule moto wa jiko la gesi katika eneo lenye madini ya bati ambayo hutumika sana kutengenezea masufuria, moto huo ulianza taratibu kupasha moto eneo hilo la bati ambayo ilisafirisha joto hadi kwenye makalio ya mzungu huyo.

            "Sasa ukaribishe ugumba katika mwili wako nakubanika makalio yako hadi korodani zako mpaka utapoongea ukweli" Norbert alimwambia yule mzungu huku akitabasamu kama ilivyo kawaida akiwa anatesa wahalifu.

    Madini ya bati(aluminium) ambayo hushika joto kwa haraka yalishika joto kama ilivyo kawaida yake, taratibu joto hilo likaanza kupamba likafika katika kiungo laini ndani ya mwili  mwanaume kisichohitajika joto kali kwa ajili ya kulinda seli za manii. Moto huo ulikuwa umeleta joto ambalo lilifika kwenye korodani kwa haraka, lilianza kuwa kama joto la kawaida na hatimaye likawa joto lenye kuumiza ngozi ya korodani ambayo ilishindwa kustahimiliwa na mzungu huyo hadi akapiga kelele akiyadhihirisha wazi mapengo yaliyojaa baada ya  kung'olewa meno na Moses.

     Ukomandoo wa mzungu huyo uliisha papo hapo mbele ya kuchomwa kwa mwenyekiti wa mwili wake, alizidi kupiga kelele huku akijaribu kufurukuta lakini kamba ngumu pamoja na vyuma alivyofungwa mikinoni na miguuni zilimzuia kufanya hivyo. Alizidi kuoiga kelele huku akimtazama Norbert lakini Norbert hakuonesha kuguswa na maumivu, alikuwa akitabasamu tu huku akimtazama.

           "Nimetumwa na mabosi wangu Sir Shaw na Don Ahmed kuja kuwamaliza vikwazo vyote ili nchi iweze kupinduliwa" Mzungu huyo aliongea kwa nguvu akasababisha Norbert ainuke aende kuzima jiko la gesi.

          "Kwa lengo gani hayo mapinduzi yafanyike" Norbert aliuliza.

            "Lengo lake ni kupitisha ushoga ambao rais wa nchi aligoma kusaini mkataba wake kisha akasababisha ipite sheria ya kuzuia ushoga, aaagh!  Tulitakiwa tuwaue nyinyi halafu nchi ipinduliwe watu walazimishwe kwa lazima kuukubali ushoga" Mzungu huyo aliongea huku akiwa bado ana maumivu.

          "Ok wakubwa wenu hapa nchini ni nani na nani?" Norbert aliuliza

           "Filbert Ole, Liutenant General Ibrahim na Wilson Ole  aaargh!" Mzungu alizidi kuongea kwani tayari alikuwa ameishiwa ujanja wote kwa maumivu aliyoyapata.
"Huo mpango ulianzia wapi?" Norbert aliuliza.

           "Umeanzia kwa wakubwa ambao siwafahamu waliwapa pesa mabosi wetu aaaargh! Walipewa dola milioni 600 ambazo Rais wenu alizikataa kusaini mkataba kupitisha mpango huo"

           "Kiongozi gani aliyewapa maelekezo yote na ni wapi alipo?" Norbert aliuliza swali ambali halikujibiwa na Mzungu huyo aliyekuwa akipiga vitunu vya maumivu  Kimya chake kilipozidi alimuambia,"niwashe tena jiko siyo".

            "Mzee Filbert Ole ndiye alitupa maelekezo baada Mnadhimu mkuu wa jeshi L.J Ibrahim kumpa kazi Belinda  ili achelewe kutoka"

           "Kwa sasa yupo wapi Filbert Ole?"

           "Sipajui panaitwaje  alipoila ni Peninsula eneo katika jiji hili"

       Kauli ya mzungu huyo iliwafanya Norbert na Moses watazamane kwa muda kisha wakaafikiana jambo kwa ishara, Moses alirudi alipokuwa amesimama M.J Belinda na Norbert alimpandisha suruali juu yule mzungu akatoka.


****

     Gari waliyopanda Santos,Thomas na Wilson ilisimama kwa ghafla mbsle ya gari ya Wilson ambayo Benson aliichukua, wote kwa pamoja walishuka ndani ya gari waliyokuja nayo wakaenda hadi ilipo gari ya Wilson. gari hiyo waliikuta inawaka ikiwa haijazimwa huku taa za mbele za gari hiyo zikimulika lango la kuingilia nyumbani kwa Leopard Queen. Walifungua kwa pamoja milango ya gari hiyo wakakuta ipo wazi yote haikubanwa, Benson pekee ndiyo hakuwepo ndani ya gari hiyo lakini kila  kitu kilikuwepo.

    Hapo walitambua kwa asilimia zote kwamba Benson atakuwa ameenda ndani ya nyumba hiyo na si vinginevyo, wote kwa pamoja waliuendea lango wa nyumba hiyo wakajaribu kulifungua lakini haukufunguka. Lango ulikuwa umefungwa kwa ndani hali iliyowalazimu waruke ukuta ili waingie kimyakimya, waliruka ukuta wakatua sehemu yenye bustani ya maua kisha wakajongea taratibu kuufuata mlango wa mbele wa kuingia ndani ya nyumba ambao upo kibarazani.

   Bastola zao zikiwa zimeelekezwa mbele baada ya kuzichomoa kiunoni mwao walisonga mbele hadi mlangoni, sauti ya kilio cha ndiyo  Benson ndiyo iliwapokea walipofika barazani ingawa haikuwashawishi washushe bastola waingie mithili ya Ng'ombe anaingia sehemu ya kuchinjia. Walifungua mlango wa nyumba kwa tahadhari  na wakaingia ndani ya nyumba kwa kuelekeza midomo ya bastola zao, waliingia hadi sebuleni ambapo walimkuta Benson akiwa amepiga magoti ameukumbatia mwili wa pscha wake Benjamin ukiwa unavuja damu.

   Benson hakujali uwepo wa vipande vya vioo yeye aliweka magoti eneo lenye vioo ambavyo vilikuwa vinamkata kwenye magoti, alikuwa akilia kama mtoto mdogo wala hakujali damu ambazo zilikuwa zikimchafua. Pembeni walimkuta Leopard Queen(Josephine) akiwa hajitambui kutokana na kutokwa na fahamu, hali waliyoikuta humo ndani iliwafanya wote wabaki wakiutazama mwili wa Komandoo wao mwenye ujuzi wa hali ya juu kushinda wao ukiwa umekumbatiwa na komandoo mwingine mwenye ujuzi zaidi.

   Benson katika kulia huko hakuwa ametambua ujio wa wenzake na alipotambua  aliwatazama kwa macho yake yaliyokuwa mekundu mithili matunda damu mbivu, machozi yalikuwa yakimtoka katika macho hayo ambayo yanatambulika kwa kuwa na hisia ngumu ambazo siyo rahisi kulia hapo  hisia zote zililainika kwa kuondokewa na ndugu yake wa damu.

           "Aaaaaaaargh! N001 sitokuacha mzima nikikutana na wewe, utalipia damu ya ndugu yangu" Benson aliongea kwa hasira huku akiuma meno yake, uchungu wa kuuliwa ndugu yake ulikuwa ukimuuma huku akisahau kwamba yeye ni hodari sana wa kuua baba,mama, kaka na dada wa wenzake. Ama kweli nyani haoni kundule ila anaona ya wenzake tu, Benson aliendelea kulia kwa uchungu baada ya kutoa maneno hayo ya kulipiza kisasi kwa N001 ambaye ametembelea nyumba hiyo pasipo kuacha alama ambayo ni rahisi kutambulika. 

      Wilson aliacha kumtazama Benson kwa huruma kutokana na jinsi anavyolia na alianda  kumtazama Leopard ambaye hakuwa na fahamu, alimtazama uzima kama upo kwa haraka na hapo tabasamu la hafifu matumaini likajaa katika uso wake.

                "Leopard Queen ni mzima jamani" Wilson aliwaambia wenzake huku akiharibu kumuinua, Thomas alikuja kwa haraka akasaidiana naye kumuinua na wakaenda kumlaza kwenye kochi wakiwa hawamjali Benson aliyekuwa akilia kama mtoto mdogo.

      Huduma ya kwanza kwa Josephine ilianza kutolewa kwa haraka huku mawasiliano yakifanywa kwa wakubwa zao, ndani ya dakika kadhaa tayari walikuwa wameshasambaza mawasiliano kwa wenzao wote ingawa waligwaya zaidi katika kusambaza taarifa hiyo. Kugwaya kulitokana na Wilson kuipiga namba ya mzungu aliyekuwa yupo chini ya kina Norbert ili ampatie taarifa, maneno aliyoyasikia kwenye simu hiyo yalimfanya aibamize chini kwa nguvu simu yake ya kisasa aliyoinunua kwa gharama.

             "Aaaargh! N001 Tenaa!" Wilson aliongea kwa ghdhabu pasipo kuijali simu yake ambayo ilikuwa ishagawanyika vipande, sauti yake ilimfanya Benson auachie mwili wa ndugu yake akasimama kwa ghafla aliposikia jina la muuaji wa ndugu yake linatajwa.

             "Yuko wapi?!" Benson aliuliza kwa hasira.



*wanalia na kusaga meno
*shimo wamechimba wametumbukia


TUKUTANE  TENA JUMATATU PANAPO MAJALIWA YA KILA HALI NA MALI.



HAIRUHUSIWI KUNAKILI RIWAYA HII KWA NAMNA YOYOTE PASIPO RIDHAA
YA MTUNZI




No comments:

Post a Comment